VYAMA TISA VIKICHUKUA FOMU UBUNGE MOSHI MJINI


MOSHI-KILIMANJARO.

Vyama tisa vya siasa vyenye usajili wa kudumu kati ya 18,vimechukua fomu kuwania kiti cha ubunge jimbo la moshi mjini katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi oktoba mwaka huu.

Vyama hivyo ni Chama cha Mapinduzi (CCM), Chama cha wananchi (CUF), CCK, NRA, TLP, MAKINI, SAU, AAFP na Chama cha CHAUMA.

Msimamizi wa uchaguzi Jimbo la Moshi mjini Sifael Kulanga, aliyasema hayo Agosti 25,2025 wakati wa zoezi la uchukuaji na urejeshaji wa fomu likitarajiwa kuhitimishwa Agosti 27 saa kumi jioni.

Mgombea Ubunge Jimbo la Moshi mjini kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Ibrahim Shayo maarufu kwa jina la (Ibra Line) ni miongoni mwa wagombea waliochukua fomu kwenye Tume hiyo. 

Akizungumza mara baada ya kuchukua fomu, Shayo alisema anakishukuru chama chake kwa kumwamini na kumteua kupeperusha bendera ya chama hicho. 

"Hakuna siku nimekuwa na furaha kama ya leo, namshukuru sana Mwenyekiti wangu wa CCM Taifa na Kamati yake kwa kuniteua kugombea nafasi hii, niko tayari kushirikiana na wana Moshi kuhakikisha chama kinapata ushindi",alisema. 

Alisema kazi iliyopo yake kwa sasa ni kwenda kushirikiana na viongozi wa chama hicho ili kushinda Uchaguzi Mkuu na kuwaletea maendeleo wananchi wa Moshi. 


Shayo, alisisitiza ushirikiano kutoka kwa makada wenzake waliojitokeza kuomba ridhaa ya chama hicho kuwania kiti hicho lakini kura hazikutosha.

Aidha alitangaza kuvunjwa kwa makundi yote na kuelekeza nguvu ya pamoja kuhakikisha jimbo hilo linaendelea kuwa mikononi mwa chama cha Mapinduzi.

Katika zoezi hilo la uchukuaji wa fomu Shayo alisindikizwa na makada wenzake akiwamo aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo Priscus Tarimo. 

Akizungumza mbele ya umati wa wanachama wa CCM nje ya jengo la Halmashauri ya Manispaa ya Moshi, Priscus alisema ndani ya CCM hakuna kununiana.

Alisema wao kama wana CCM wanajukumu moja la kuhakikisha kura za Rais,Wabunge na Madiwani zinamwagika.





Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.