UHAMIAJI YATAKIWA KUONGEZA JUHUDI UKUSANYAJI MAPATO KUPITIA VIZA

MOSHI-KILIMANJARO

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Dkt. Maduhu Kazi, amewataka Watumishi wa Idra ya Uhamiaji kuongeza jitihada katika ukusanyaji mapato yatokanayo na viza kwa wageni wanaoingia nchini , ili kuunga mkono juhudi za serikali katika kukuza mapato ya Taifa.

Dk. Kazi alitoa kauli hiyo jana mjini Moshi wakati wa ufunguzi wa kikao cha 18 cha Baraza la Wafanyakazi wa Idara ya Uhamiaji (TUGHE) kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Chuo cha Kikanda cha Uhamiaji (TRITA) mjini Moshi mkoani Kilimanjaro.

Katika hotuba yake Dkt. Kazi alisema licha ya jukumu walilopewa Idara ya Uhamiaji ya kulinda mipaka ya nchi pamoja na vipenyo mbalimbali, bado wana wajibu wa kuhakikisha mapato yote yatokanayo na utoaji wa viza kwa wageni yanakusanywa kimalifu.

"Ni kweli kazi yenu kubwa ni kulinda mipaka ya nchi, lakini pia mnalo jukumu la msingi la kuhakikisha mapato ya serikali yanapatikana kupitia ada za viza  kwani hili ni eneo muhimu sana ambalo haliwezi kubezwa,"alisema Dkt. Kazi.

Aliongeza kuwa mapato hayo ni sehemu ya ya vyanzo vya ndani vinavyoiwezesha serikali kutekeleza majukumu yake mbalimbali ya kuwahudumia wananchi, hivvyo ni wajibu wa kila mtumishi kuhakikisha anatekeleza jukumu hilo kwa weledi na uzalendo.Kwa upande wake Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Nchini  Dkt. Anna Makakala, alisema lengo la kikao hicho cha 18 cha Baraza la Wafanyakazi Tawi la Uhamiaji, ni kujadili utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2024/2025 na kupitisha bajeti ya mwaka 2025/2026.

"Tuna mshukuru sana Rais Samia Suluhu Hassan maoteo ya bajeti ya mwaka 2024/2025 tumeyona, kumekuwa na maboresho makubwa sana kwani hata bajeti imeongezeka ,"alisema Dkt. Makakala.

Dkt. Makakala alitoa wito kwa bajeti mpya kuzingatia maslahi ya wafanyakazi ili waweze kutekeleza majuikumu yao kwa ufanisi, huku akisisitiza umuhimu wa watumishi kutimiza wajibu wao ipasavyo  wanapodai maslahi yao.Aidha Kamishna Jenerali DKt. Makakala, alieleza kuwa ushirikishwaji wa Wafanyakazi katika mchakato wa bajeti ni muhimu, hasa katika kuelekea Bunge la bajeti la mwaka 2025/2026 ili kuhakikisha mchango wao unazingatiwa.

Naye Mwenyekiti wa (TUGHE) Taifa Joel Kaminyonge, alisema kikao hicho kimelenga kupitia utekelezaji wa majukumu ya Idara hiyo na changamoto zilizopo pamoja na kutoa mapendekezo ya maboresho katika utendaji kazi.

"Tutapitia utekelezaji wa bajeti ya mwaka uliopita na kuhakikisha bajeti ijayo inajibu changamoto zilizopo kwa watumishi,"alisema.




Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.