MBUNGE NDAKIDENI ATOA MICHE YA MIGOMBA 10,000 KWA KATA 14 ZILIZOKO UKANDA WA MILIMANI


MOSHI-KILIMANJARO

Ndizi ni moja ya mazao muhimu ya chakula na biashara katika Afrika Mashariki, katika maeneo mengi ya kanda hii, ndizi hutumika kama chakula kikuu kwa familia nyingi, na pia ni chanzo muhimu cha kipato kwa wakulima.

Katika maeneo ya vijijini, ndizi za kupika, kama vile matoke, ni chakula cha kila siku, ambacho huliwa kwa namna mbalimbali: kuchemshwa, kukaangwa, au kupikwa kwa mchuzi.

Ndizi si tu kwamba ni chakula kinachoweza kutumika kwa haraka na kwa urahisi, bali pia ni chanzo cha lishe bora, zina kiwango cha juu cha wanga, vitamini muhimu kama vile vitamini C, na madini kama potasiamu, ambayo ni muhimu kwa afya ya moyo na kudhibiti shinikizo la damu.

Kwa upande wa biashara, ndizi ni zao ambalo lina mchango mkubwa kwa Wakulima, kwa wengi wao, ndizi ni chanzo kikubwa cha kipato.

Katika kulitambua hilo Mbunge wa Jimbo la Moshi Vijijini Prof. Patrick Ndakidemi ametoa miche 10,000 ya migomba kwa kata 14 zilizoko ukanda wa milimani ili kuhakikisha zao hilo linaendelea kupatikana kwa wingi.

Hayo aliyasema Aprili mosi, 2025 katika hafla fupi ya makabidhiano ya miche hiyo, kwa viongozi wa CCM kutoka kata 14 za Moshi vijijini ambapo zao hilo limekuwa likilimwa kwa kiasi kikubwa.

Prof. Ndakideni alisema kuwa lengo la kutoa miche hiyo ni kuhamasisha uzalishaji wa ndizi na kuongeza tija kwa wakulima wa milimani.

Alisema; kilimo cha ndizi kina manufaa makubwa katika kuboresha lishe, kuongeza kipato cha familia, na kuchangia katika uchumi wa jamii.

“Jimbo la Moshi Vijijini hususan ukanda wa milimani una ardhi na mazingira bora kwa kilimo cha migomba na mbegu niliyowapa itaenda kuongeza uzalishaji ambapo mkungu mmoja unaweza kufikisha kilo 150 hadi 200 ukilinganisha na migomba iliyopo kwa sasa ambayo wanavuna kati ya kilo 10 hadi 50.”alisema,

Aliongeza kuwa “Zao hili linachangia kwa kiasi kikubwa katika uchumi wa familia na jamii, katika baadhi ya maeneo, ndizi hufanyika kama biashara kubwa ambayo inategemea uzalishaji na usafirishaji wa ndizi kwenda katika miji mikubwa na hata nchi nyingine,”alisema Prof. Ndakidemi.

Alifafanua kuwa wakati wa kampeni mwaka 2020 aliwaahidi wananchi wa jimbo hilo kuwaletea migomba, ambapo aliwasiliana na taasisi ya Kimataifa ya The International Institute of Tropical Agriculture (IITA)  ambayo ilimpatia ufadhili wa mbegu hizo kupitia kwa Profesa Rony Swenen.

Aidha alisema kuwa Serikali inaandaa mpango maalumu utakaofanya zao la ndizi kuwa zao la kibiashara hivyo wakulima kutoka maeneo mbalimbali ya jimbo hilo watanufaika na miche hiyo ili ile dhima iliyokusudiwa iweze kutimia.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti mara baada ya kukabidhiwa miche hiyo baadhi ya viongozi wa CCM katika kata hizo akiwemo Katibu wa Jumuiya ya Wazazi Andrew Mwandu, Katibu wa CCM Kata ya Mbokomu Sofia Mshiu na Mwenyekiti wa CCM Kata ya Old Moshi Mashariki Ronald Tenga walisema mbegu hizo zitasaidia wakulima kuzalisha kwa tija na kuongeza mapato ya kaya.


Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.