MOSHI.
Wakati Dunia ikiombeleza kifo cha Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani Papa Francisco, Wadau wa mazingira mkoani Kilimanjaro wameamua kumuenzi kiongozi huyo kwa kupanda miti kwenye uwanja wa Uhuru Park ulioko Manispaa ya Moshi, mkoani humo kama ishara ya kumuenzi kwa kazi kubwa aliyoifanya ya utunzaji wa mazingira.Mraribu wa zoezi hilo Daniel Mvungi; alisema wameamua kupanda miti aina mbalimbali ya matunda ili kuenzi kazi nzuri aliyoifanya Papa Francisco ya kutunza mazingira wakati wa uhai wake.
Mvungi ambeye ni Mwenyekiti wa taasisi isiyo ya kiserikali ya (Kibo Sports Club), inayojishughulisha na michezo na mazingira alisema, waliendesha zoezi hilo la upandaji wa miti kwa ushirikiano wa karibu na taasisi ya mazingira ya Mongola Environment Conservation Group.
"Nitoe rai kwa watu wote duniani wenye kujali mazingira kumuenzi Papa Francisco kwa kuboresha mazingira maeneo wanayoishi", alisema na kuongeza, utunzaji wa mazingira ni moja ya urithi ambao Papa Francisco alituachia.
Kwa upande Mkufunzi wa masuala ya Utamaduni ambaye pia ni Mjumbe wa taasisi ya Mongola Environment Conservation Group Gasper Shirima Gorila, kwa jina maarufu kama Mtikisa Misitu, alitoa rai kwa wananchi kutumia mvua zinazoneysha kila mwaka kupanda miti ili kuboresha mazingira.
"Kila mwaka tunajaliwa kupata mvua za masika na za vuli lakini maji ya mvua huishia chini tu; ni vyema sasa kuanzia sasa tukajenga utamaduni wa kutumia mvua hizi kupanda miti kila mwaka", alisema, na kuongeza, hii pia itakuwa ni njia nzuri ya kumuenzi Papa Francisco ambaye wakati wa uhai wake alijikita katika kuboresha mazingira.
Baadhi ya washiriki wa zoezi hilo John Mushi, Amina Rashid na Assenga, walieleza kufurahishwa kwao na hatua ya Kibo Sports Club na Mongola Environment Conservation Group, wakisema imewapa motisha ya kushiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi wa mazingira.