MOSHI-KILIMANJARO.
Wafanyabiashara mkoa wa Kilimanjaro wamemshukuru Rais Dk. Samia
Suluhu Hassan kwa kuboresha mazingira ya ulipaji kodi nchini.
Shukrani hizo walizitoa Februari 19,2025 mkoani hapa, wakati wa
hafla ya utoaji wa Tuzo kwa Walipa kodi bora mkoani Kilimanjaro kwa mwaka
2023/24, hafla iliyofanyika mjini Moshi, mkoani hapa.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kupokea Tuzo
hiyo kutoka TRA Mkurugenzi wa Kampuni ya Mafuta ya (Kifaru Oil Investment Ltd)
kutoka Wilayani Mwanga Suleiman Mfinanga ameipongeza TRA kwa kuanzisha Tuzo ya
walipa kodi bora ambayo alisema imechangia wafanyabiashara wengi kulipa kodi
kwa hiari.
“Tunaishukuru sana serikali kwa kutuwekea mazingira bora ya
kufanya biashara, lakini pia na elimu ya mlipa kodi inayotolewa na TRA
imetuwezesha sisi wafanyabiashara kulipa kodi kwa hiari yetu pasipo kuweko na
msuguano,”alisema Mfinanga.
Alisema utaratibu ambao TRA imekuja nao wa kuwa zawadia Tuzo imewapa
moyo wafanyabiashara wengi kujitokeza na kulipa kodi kwa hiari jambo ambalo
litaiwezesha Serikali kutekeleza mipango yake ya kimaendeleo.
“Walipa kodi kila siku wanakuja wapya, tuwaombe Mamlaka ya
Mapato Tanzania (TRA) kuongeza kasi ya utoaji wa elimu ya mlipa kodi kila
wakati ili wasiwe wanawapiga faini wafanyabiashara.”alisema Mfinanga.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kampuni ya Rock Blocks ya Wilayani
Rombo Fabian Woiso, alisema tuzo hiyo ni muhimu kwa wafanyabiashara kutokana na
ukweli kuwa inawapa wafanyabiashara nafasi ya kukutana na uongozi wa Serikali
na kupata elimu mpya kila mwaka kuhusu umuhimu wa kulipa kodi.
“Hatua hii itatujengea sisi wafanyabiashara na wananchi wote kwa
ujumla kuwa na moyo wa kulipa kodi jambo ambalo alisema litaongeza idadi ya
walipa kodi wengi na hivyo kuongeza mapato ya Serikali kupitia makusanyo ya
kodi”, alisema Woiso.
Mkuu wa Wilaya ya Moshi Godfrey Mnzava, aliwapongeza wafanyabiashara kwa kitendo hicho cha kizalendo cha kulipa kodi kwa hiari na kwa wakati.
“Niwapongeze sana wafanyabiashara wa mkoa wa Kilimanjaro kwa kuunga mkono juhudi za serikali za awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ambaye ameendelea kuhimiza kila mtu anayeshtahili kulipa kodi alipe kodi stahiki lakini kwa hiari na kwa wakati.”alisema DC Mnzava.