Sh bilioni 1 zatengwa ujenzi wa uwanja wa Majengo

MOSHI.

Halmashauri ya Manispaa ya Moshi, mkoani Kilimanjaro, imetenga jumla ya Sh bilioni 1 kwa ajili ya maboresho ya uwanja wa michezo wa Majengo.

Lengo kuu la mpango huo ni kutumia fursa ambazo zitatokana na Tanzania kuwa mwenyeji mwenza wa michuano ya AFCON mwaka wa 2027.

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi wa halmashauri hiyo Mwl. Mwajuma Nasombe, wakati wa kikao cha Baraza cha bajeti ya halmashauri hiyo kwa mwaka wa fedha wa 2025/26 kilichofanyika, mwishoni mwa wiki.

“Fedha hizi ni ziada ya Sh milioni 600 ambazo tayari zilishatumika katika ujenzi wa uwanja huo ambao umechangia kwa kiasi kikubwa kukua kwa michezo haswa mpira wa miguu Manispaa ya Moshi na mkoa wa Kilimanjaro kwa ujumla”, alisema.

Mwl. Nasombe alisema mbali na fursa hiyo pia uamuzi huo umelenga kuunga juhudi za Rais Samia Suluhu Hassan zinazolenga kuiinua sekta ya michezo hapa nchini ambayo pia imepelekea Tanzania kuandaa michuano ya AFCON kwa Ushirikiano na Mataifa mengine ya Afrika Mashariki ya Kenya na Uganda.

“Fursa ambayo tunataka kuichangamkia kupitia uwekezaji wa uwanja wetu wa Majengo ni ile ya timu ambazo zitashiriki michuano ya AFCON mwaka 2027  kwenye kituo cha Arusha wauutumie na uwanja wetu wa Majengo kwa ajili ya mazoezi yao”, alisema.

“Timu zitakazoshiriki michuano hiyo zitahitaji viwanja vya kufanyia mazoezi hivyo uwanja wa Majengo utakuwa na fursa ya kupata walau timu moja ambayo itautumia na hivyo kuongeza mapato ya hamashauri yetu”, alisema.

Aidha mkurugenzi huyo alitoa wito kwa wafanyabiashara wa Mkoa wa Kilimanjaro na wale wa Mikoa ya jirani kujitokeza kuunga mkono juhudi za halmashauri hiyo katika maboresho ya uwanja huo ili nao wanaufaike kupitia fursa hiyo ikiwemo kujitangaza kupitia uwanja huo.

Alisema “Fursa hii ni muhimu ambayo inaweza kuchangia biashara zao haswa ikitiliwa maanani ya kuwa mchezo wa mpira wa miguu ni maarufu na matangazo yake hufika mbali kupitia michuano mbalimbali ya soka ya ndani na yale ya Kimataifa”, alisema.

Kwa upande wake Meya wa halmashauri ya Manispaa ya Moshi Mhandisi Zuberi Kidumo alisema kuwa gharama za ukarabati wa uwanja huo unatokana na makusanyo ya Sh bilioni 10 ambayo yatakuwa ni mapato ya ndani ya halmashauri hiyo kwa mwaka wa fedha wa 2025/26.

“Maboregso ya uwanja huu yatahusu pamoja na mambo mengine uwekaji wa viti vya watazamaji, ufungaji wa taa za uwanjani, nyasi bandia pamoja na miundombinu ya kuingia na kutoka uwanjani”, alisema Mhandisi Kidumo.

Nao baadhi ya wadau wa michezo Manispaa ya Moshi, wameupongeza uongozi wa Manispaa hiyo  kwa uamuzi huo ambao walisema utaendelea kuitangaza halmashauri hiyo  Moshi kupitia sekta ya michezo.

“Uweko wa uwanja huu ni hatua kubwa ya kimaendeleo kutokana na ukweli kuwa Manispaa ya  Moshi haikua na uwanja na badala yake walikuwa wanalazimika kutumia viwanja vya taasisi mbalimbali pale mahitaji yanapotokea”, alisema Abdalla Mtwenge mdau wa michezo Moshi Mjini.

Mtwenge alisema mbali na kutumika kwa ajili ya michezo aina mbalimbali uwanja huo pia utatoa fursa ya wafanyabiashara mbalimbali wakiwemo wale wa vyakula na usafirishaji kuongeza mapato yao wakati wa mashindano mbalimbali yakayofanyika uwanjani hapo.

Kwa upande wake mdau mwingine wa michezo Wilson Enock alisema uamuzi wa Manispaa ya Moshi kuuboresha uwanja huo kutaongeza mapato ya halmshauri na fursa kwa wenyeji kuboresha hali zao za kiuchumi.


Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.