Timu ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia (Mama Samia Legal Aid Campaign) imefanikiwa kutatua mgogoro wa ardhi uliodumu miaka zaidi ya 30 na thatimaye kufikia tamati.
Hayo yalijiri Februari 8,2025 baada ya timu hiyo kumkabidhi mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro Nurdin Babu, taarifa ya utendaji kazi ya Huduma ya Msaada wa Kisheria bure kupitia "Mama Samia Legal Aid Campaign".
Akizungumza na Waandishi wa habari nje ya Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro Wakili wa Kujitegemea kutoka Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Dk. Belinda Chepchumba, alisema kupitia kapeni hiyo waliweza kutatua migogo miwili ya ardhi Kata ya Mabogini Wilaya ya Moshi Vijijini ambayo imedumi kwa miaka mingi.
“Kupitia kampeni hii ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia (Mama Samia Legal Aid Campaign) tuliweza kufika Kata ya Mabogini iliyoko halmashauri ya Wilaya ya Moshi Vijijini, tuweza kutatua mgogoro wa ardhi, uliodumu kwa miaka zaidi ya 30, lakini pia tumetatua mgogoro mwingine wa ardhi uliodumu kwa miaka minne.”alisema Dk. Chepchumba.
Dk. Chepchumba ambaye pia ni Mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam shule ya Sheria, alisema kupitia kampeni hiyo waliweza kuzifikia kata 10 na vijiji 30 zilizoko halmashauri hiyo na kufanikiwa kutatua migogoro 105.
“Migogoro ambayo ilijitokeza kwa wingi ni migogoro ya ardhi, ukatili wa kjinsia pamoja na masuala ya ndoa, ipo migogoro ambayo tuliweza kuitatua lakini pia kuna migogoro ambayo hatukuweza kuitatua hivyo, itaendelea kutatuliwa na Wanasheria wetu wa TLS kwa kusikilizwa na kuhudumiwa bure kabisa.”alisema.
Akikabidhi taarifa hiyo kwa Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro Mrakibu
wa Huduma wa Msaada wa Kisheria, Wizara ya Katiba na Sheria Murumbe James
Daudi, alisema hoja zaidi ya 700 walizipokea na kuzitatua, hoja 21 ziliweza kupata huduma, migogoro 94 ikiwa ya viwandania na migogoro
zaidi ya 600 itaendelea kufanyiwa kazi kupitia kwa Mawakili TLS.
“Tunaipongeza sana Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa halmashauri za mkoa huo, kwani kila ambako timu hizi zilipita hatukuweza kupata changamoto yoyote ushirikiano ulikuwepo wa kutosha.”alisema.
Kwa upande wake Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro Nurdin Babu alisema wananchi 121,349 walijitokeza kutoa changamoto zao mbalimbali zilizokuwa zinahusu masuala ya Kisheria.
“Nimepokea taarifa ya
Mawakili na Wanasheria kutoka Ofisi ya Katiba na Sheria ambayo ilikuwa
inaendesha zoezi kwa siku 10 katika mkoa wetu kupitia Kampeni ya Mama Samia
Legal Aid Campaign ,” alisema.
Babu alisema katika
ripoti aliyokabidhiwa hoja 646 hazikuweza kutatuliwa na kwamba amekabidhiwa ili aweze kuzifanyia kazi.
Alisema kwenye hoja hizo nyingi
ni za migogoro ya ardhi, ukatili wa kijinsia, ulawiti na utekelezaji wa watoto
ambao umeonekana kwenye maeneo mengi ya mkoa huo.
Kampeni ya Huduma wa Msaada
wa Kisheria ya Mama Samia (Mama Samia Legal Aid Campaign) ilizinduliwa mkoa wa
Kilimanjaro Januari 29 mwaka huu , ikiwa imejikita zaidi katika kutoa elimu ya
kisheria kwa wananchi hususan katika masuala ya ukatili wa kijinsia, migogoro
ya ardhi, mirathi, usuluhishi wa migogoro ya ndoa.





