Waziri wa Afya ampongeza Dk. Subi kwa usimamizi mzuri wa miaradi ya maendeleo ya kimkakati

Waziri wa Afya Jenista Mhagama (kulia), akimpongeza Mkurugenzi wa Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto (KIDH), Dkt. Leonard Subi, kwa usimamizi mzuri wa miradi ya maendeleo ya kimkakati iliyowezesha kuboresha sekta ya afya hospitalini hapo.

KIBONG’OTO-SIHA.

Serikali imesema inatambua mchango mkubwa unaotolewa na Mkurugenzi wa Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto (KIDH), Dkt. Leonard Subi na menejimenti yake  jambo ambalo limewezesha kuboresha sekta ya afya hospitalini hapo na hivyo kuipa heshima nchi ya Tanzania kwenye tasnia ya afya ulimwenguni kote.

Waziri wa Afya Jenista Mhagama, alitoa pongezi hizo Januari 10,2025, wakati akizindua Bodi mpya ya uongozi ya hospitali hiyo, hafla iliyofanyika hospitalini hapo.

Alisema hospitali ya Kibong’oto, imetoa mchango mkubwa kupitia tafiti zake mbalimbali ambazo zimechangia pamoja na mengine kupunguza muda wa matibabu kwa wagonjwa wa Kifua Kikuu, kutoka miaka miwili hadi kufikia miezi 9 lakini pia wameweza kupunguza matumizi ya dawa nyingi kwa muda mrefu katika kutibu ugonjwa huo.

“KIDH imetoa mchango mkubwa uliopelekea kuondolewa kwa tiba ya Kifua Kikuu kwa kutumia sindano; mafanikio haya yamelipatia Taifa heshima kubwa Kimataifa”alisema. 

Alisema kuwa matumizi ya sindano kwa muda mrefu na hata yale ya dawa, yalikuwa yakipelekea wagonja wengi kushindwa kumalizia muda wa matibabu waliyowekewa na hivyo kusababisha ugonjwa huo kufikia hali ya usugu, hali ambayo ilimfanya mgonjwa wa Kifua Kikuu kuwa na hali mbaya zaidi.

Waziri  Mhagama, alisema kuwa kwa kipindi cha miaka mitatu ambayo Dk. Subi amekuwepo katika hospitali hiyo, yako mageuzi makubwa aliyoyafanya, ikiwemo usimamizi mzuri wa fedha za miradi ya maendeleo inayotekelezwa ndani ya hospitali hiyo.

“Ndugu zangu mnyonge mnyongeni haki yake mpeni,  kwa kipindi cha  miaka mitatu sisi serikali, tumeshuhuduia mageuzi makubwa ya kimaendeleo na kimkakati yanayofanyika kwenye hospitali hii, imedhihirisha ni aina gani ya kiongozi tuliyenaye anayesimamia hospitali hii, lakini pia na aina ya watumishi ambao wanafanya kazi katika hospitali ya Kibong’oto,”alisema Waziri Mhagama.

Akizungumzia Bodi hiyo mpya, Waziri Mhagawa alitoa rai kwa uongozi huo kuendelea kushirikiana na menejimenti ya hospitali hiyo ili kuendeleza mafaniko ambayo yamepatikana.

Akiwasilisha taarifa ya hospitali hiyo, Mkurugenzi wa KIDH Dk. Leonard Subi, alisema kuwa mafanikio yaliyopatikana hospitalini hapo yametokana na tafiti mbalimbali zinazofanwa na wataalam walioko hospitalini hapo.

“Tunaishukuru Serikali kwa mchango wake mkubwa kwa hospitali yetu hii,  zikiwemo fedha zaidi ya Sh bilioni 22.5 fgedha ambazo zimepelekea ujenzi wa Maabara ya Afya ya Jamii pamoja na ununuzi wa vifaa tiba,” alisema Dk. Subi.

Aidha Dk. Subi alisema kuwa katika mwaka wa fedha 2023/2024,  hospitali hiyo iliwahudumia jumla ya watu 36,154 na kwamba asilimia 90 ya wananchi wanaofika kutibiwa katika hospitali wanaridhika na huduma zinazotolewa na hiyo.

Aliongeza kuwa “Asilimia 75 ya wagonjwa waliotibiwa ugonjwa Kifua Kikuu Sugu (TB) wamepona na haya ni mafanikio makubwa ikilinganishwa na kiwango cha mataifa cha asilimia 63 ya wale waliopona baada ya kupata matibabu”, alisema.

Akizungumza kwa niaba ya uongozi wa Bodi uliomaliza muda wake, Mjumbe wa bodi hiyo (iliyomaliza muda wake) Daniel Sendewa aliishukuru Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kuwaamini jambo ambalo limepelekea hospitali hiyo kupata mafanikio makubwa.

“Nichukue fursa hii pia kuishukuru Serikali kwa ushirikiano wake mkubwa kwa Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto (KIDH) ambao umeifanya hospitali hii kupata heshima ndani na nje ya nchi”, alisema Sendewa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti mpya wa Bodi hiyo ambayo ni ya tatu hospitalini hapo, Prof. Muhammad Bakari Kambi aliishukuru Serikali kwa kuwaamini na kisha kuwakabidhi jukumu la kushirikiana na uongozi wa KIDH kwa ajili ya kuboresha sekta ya afya.

Aidha aliupongeza uongozi wa bodi iliyomaliza muda wake kwa kazi nzuri zilizopelekea KIDH kustawi na hali iliyopelekea (KIDH) kuwa uendelevu, na hivyo kupelekea uteuzi na hatimaye uzinduzi wa bodi mpya.

Miongoni mwa Wajumbe wa Bodi hiyo walioteuliwa na Waziri wa Afya ni pamoja na Dk. Mary Mayige, Adelmarsi A. Ndangasani, Dk. Stanley P. Chattanda, Mauldid N. Nyamlenganwa, Prof. Kajiru G. Kajiru na Dk. Ntuli Kapologwe.



















Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.