Wananchi Korogwe waipongeza PBWB kuanza kuweka alama za utambuzi wa maeneo yenye vyanzo vya maji

KOROGWE-TANGA.

Wakazi wa Wilaya ya Korogwe na Lushoto Jijini Tanga, wameipongeza Bodi ya Maji Bonde la Pangani (PBWB) kwa kuanza kuchukua hatua za kuweka lama za kudumu za utambuzi wa maeneo yenye vyanzo vya maji ili kuvinusuru na uharibifu unaosababishwa na shughuli za kibinadamu.

Akizungumza mmoja wa wakazi wa wilaya hiyo James Kaniki, alisema serikali kuanza kuchukua hatua za utambuzi wa maeneo yenye vyanzo vya maji na kuweka alama ni jambo zuri, kwani itasaidia kuvilinda vyanzo vya maji ili kuendelea kuwa na uhakika wa maji safi na salama wakati wote.

“Hatu za Bodi ya Maji Bonde la Maji Pangani, kuweka alama za kudumu zitasaidia sana kuzuia shughuli za kilimo na ufugaji ambazo zinaathiri kwa kiwango kikubwa maeneo yenye vyanzo vya maji,”alisema Kaniki.  

Mkurugenzi wa Bodi ya Maji Bonde la Pangani Mhandisi Segule Segule; alisema kufuatia uvamizi wa vyanzo vya maji  PBWB, imeanza shughuli ya tathmini ya vyanzo ili kuweka alama za mipaka (beacons), kwa kushirikiana na viongozi wa Kata na Kijiji ili kuweza kuhifadhi chanzo cha Kwematambwe ambacho kimevamiwa na shughuli za kibinadamu pamoja na Mto Umba.

Mhandisi Segule, alisema Sheria za Usimiamizi wa rasilimali za maji namba 11 ya mwaka 2001 na Sheria  ya Usimamizi wa Mazingira namba 20 ya mwaka 2004 kifungu namba 57 ambacho kinakataza shughuli za binadamu ndani ya mita 60 kwenye vyanzo vya maji.

Akizungumza kwenye kikao cha tatu cha wadau wa Usimamizi wa rasilimali za maji kidakio cha Mto Umba Segule alisema Mkoa wa tanga una vyanzo vya maji zaidi ya 400 huku vyanzo 140 pekee ndio vyenye mipaka ya alama za utambuzi, ikiwa ni jitihada za kuwachukulia hatua za kisheria wananchi ambao wanatumia huduma za maji bila vibali maalum hali ambayo inasabisha uharibifu wa miundombinu .

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Korogwe William Mwakilema,aliwataka wananchi na wadau wote wa rasilimali za maji kufuata Sheria na kushirikiana na Bodi ya maji Bonde la Pangani kuendelea kutunza vyanzo vya maji.

“Ni kosa la mwananchi yeyote kuchepusha maji au kutumia maji pasipo kuwa na vibali maalum na adhabu inayotolewa ni kifungo cha miaka miwili hadi mitano jela na kiasi cha Sh laki 5 hadi milioni 50.”

Bodi ya Maji Bonde la Pangani inasimamia eneo bonde lenye ukubwa wa takribani kilomita za mraba 54,600 ambayo ni asilimia 93% ya Bonde zima na asilimia 7 iko Nchini Kenya inayolifanya Bonde la Pangani kuwa ni la kimataifa.

Pia Bodi ya Maji Bonde la Mto Pangani inasimamia Mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Tanga na Manyara katika Halmashauri za Wilaya takribani 24.







Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.