Mafundi rangi, ujenzi watakiwa kuutumia mfumo wa Nest kuomba kazi za ujenzi

MOSHI-KILIMANJARO.

Serikali imewataka mafundi rangi na ujenzi mkoani Kilimanjaro, kuutumia mfumo wa ununuzi wa kielektroniki wa (Nest),ili kuomba kazi za ujenzi zinazotangazwa na halmashauri.

Rai hiyo imetolewa jana na Katibu Tawala wa  Wilaya ya Moshi mkoani humo Shaban Mchomvu, wakati akifungua mkutano mkuu wa kwanza wa Chama cha Mafundi Rangi na Ujenzi (CHAMARUKI),uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Morio Hall mjini Moshi mkoani humo.

Mchomvu alisisitiza kuwa nidhamu, upeo wa kuziendea fursa hasa kupitia mitandao na majukwaa mbalimbali ni jambo muhimu kwa mafundi ili kufanikisha kazi zao na kujikwamua kiuchumi.

Aliwataka mafundi hao, kuhakikisha kwamba wanautumia mfumo wa ununuzi wa kielektroniki (NeST) kwa udailifu, uwazi na uwajibikaji ili kunufaika na fursa za ujenzi zilizopo ndani ya serikali na taasisi binafsi katika kufikia malengo yao.

“Rais Samia ameleta fedha nyingi sana za miradi ya maendeleo katika mkoa wetu wa Kilimanjaro, hata kama mkiamua leo hii kuigawana kuna miradi mingine mtaiacha, hivyo niwasisitize suala la nidhamu ya matumizi mazuri ya mitandao,”alisema Mchomvu.

Alisema kuwa umoja miongoni mwa mafundi ni jambo muhimu sana na kwamba kupitia umoja huo aliutaka uongozi wa CHAMARUKI kuhakikisha wanawahamasisha mafundi wanawake kujiunga na chama hicho ili kufikia malengo tarajiwa zikiwemo fursa za ujenzi.

Awali akizungumza Katibu Chama cha Mafundi Rangi na Ujenzi (CHAMARUKI), mkoani humo Casmiry John Toto, alisema wameanzisha chama hicho kwa lengo la kutengeneza thamani ya mafundi katika jamii na kuziendea fursa zilizopo katika sekta ya ujenzi kupitia umoja wao.

“Tunatengeneza sauti ya kuweza kuwasilisha jambo ambalo linaweza kuwa na tija katika jamii, kuondoa dhana ya kuiona sekta ya ujenzi ni kama sekta ya watu ambao hawana, lakini pia ni sehemu ya kupaza sauti kwa maslahi mapana kwa jamii na taifa kwa ujumla.”alisema Toto.

Kwa upande wake Meneja wa tawi la Azania Benk Moshi Moshi, mkoa wa Kilimanjaro Yusuf Lenga; aliwapongeza kwa kuanzisha umoja huo huku akisema kuwa  sekta ya ujenzi (mafundi) ni sekta muhimu katika maendeleo hapa nchini.

“Sekta ya  mafundi  rangi  na ujenzi ni sekta ambazo zinabadilisha maisha, mtizamo na hali za Watanzania na Taifa kwa ujumla hivyo nawapongeza sana kwa kuanzisha umoja wenu huu.”alisema Lenga.

Aliongeza kuwa “Sisi Azania Benk tunaona umuhimu wa  kushirikiana na (CHAMARUKI), kama sehemu ya jamii, tunato huduma mbalimbali ikiwemo mikopo ya kimaendeleo kwa mafundi mmoja mmoja na vikundi ambao wanaotambulika na serikali.”alisema.

Yusuph Said na Judika Evarest ni baadhi ya mafundi wanaounda umoja huo walielezea matumaini yao ya umuhimu ya kuwa na chama hicho katika kuzifikia fursa zilizopo, ambapo katika mkutano huo pia ulihudhuriwa na wafanyabiashara na wadau mbalimbali waliopo katika sekta ya ujenzi ambapo pamoja na mambo mengine wajumbe hao, walipitisha rasimu ya mapendekezo ya Katiba yao sambamba na kusomewa taarifa ya mapato na matumizi. 









Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.