Magic Builder’s International yatangaza kulipia ada watoto wa mafundi rangi na ujenzi

MOSHI-KILIMANJARO

Kampuni ya Magic Builder's International Ltd, inayojihusisha na uzalishaji wa bidhaa za ujenzi kama vile white skim wall putty, imejizatiti kuwalipia ada watoto wa mafundi rangi na ujenzi wanaosoma shule za msingi za serikali.

Hayo yamesemwa na Afisa Masoko wa Kampuni hiyo Kanda ya Kaskazini, Brighton Geofrey, katika mkutano mkuu wa Kwanza wa Chama cha Mafundi Rangi na Ujenzi (chamaruki),uliofanyika Morio Hall mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro.

Geofrey alisisitiza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya kutambua mchango wa mafundi rangi na ujenzi ambao ni wadau muhimu katika kufanikisha malengo ya kampuni hiyo.

Aliongeza kuwa kampuni hiyo imekuwa ikiunga mkono juhudi za serikali za kuboresha miundombinu ya elimu, ikiwa ni pamoja na ujenzi wa madarasa mapya na urekebishaji wa yale ya zamani.

Kwa upande mwingine, alielezea kuwa kampuni hiyo ina mipango ya kuendelea kusaidia mafundi rangi na ujenzi, na kwamba wameanzisha mpango huu katika mkoa wa Kilimanjaro kama sehemu ya michango yao kwa jamii.

Vilevile, aliwashauri mafundi hao kuendana na mabadiliko ya kiteknolojia na kujisajili kwenye mfumo wa Nest wa serikali ili kupata fursa za kazi kupitia makampuni ya vifaa vya ujenzi.

Katika hatua nyingine, kampuni hiyo pia imetangaza kuwa itaendelea kutoa zawadi kupitia bahati nasibu kwa mafundi mbalimbali katika mikoa mbalimbali nchini.





Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.