4R zilizoasisiwa na Rais Samia zimeleta mabadiliko chanya nchini

MOSHI

Waziri wa Katiba na Sheria Dk. Damas Ndumbaro, amemshukuru Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuja na Falsafa ambayo imejikita katika masuala ya maridhiano, ustahamilivu mageuzi na kujenga upya taifa, ambayo imeleta mabadiliko chanya hapa nchini.

Waziri Ndumbaro aliyasema hayo jana Mkoani Kilimanjaro, wakati wa uzinduzi wa Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya MAMA SAMIA LEGAL AID, iliyofanyika katika standi ya zamani ya mabasi mjini Moshi mkoani humo.

Alisema kupitia 4R za Rais Samia, zimeendelea kutamalaki jambo ambalo limewezesha hata kampeni ya Msaada wa Kisheria kuwa na matokeo chanya ya ya falsafa hiyo.

“Falsafa hii imejikita katika masuala ya Maridhiano (Reconciliation), Ustahamilivu (Resilience), Mageuzi (Reforms), na Kujenga upya Taifa (Rebuilding), 4R hizi zimefanya nchini kuendelea kuwa na amani,”alisema Waziri Ndumbaro.

Akizungumzia kampeni hiyo maalum Dk. Ndumbaro alisema kuwa ni matokeo ya maono aliyokuwa nayo Rais Dk Samia baada ya kubaini ya kuwa watu wengi wana kiu ya haki, jambo ambalo amesema linadhibitishwa na umati mkubwa wa watu wanaojitokeza kwenda kupata ushauri wa kisheria kila mahali kampeni hiyo inapofanyika hapa nchini.

“Serikali ya awamu ya sita iligundua ya kuwa wananchi wengi na wana kiu ya haki na ndipo Rais Dk Samia kupitia busara zake akaanzisha kampeni hii nchi nzima ili kukidhi kiu ya haki waliyonayo watu wengi haswa wale ambao hawana uwezo wa kulipia gharama za wataalam wa kisheria”, alisema.

Dk. Ndumbaro aliwapaongeza wale wote ambao wamejitokeza kupata huduma zinazotolewa kupitia kampeni hiyo jambo ambalo alisema limedhihirisha ustaarabu wa Watanzania wa kutafuta haki kupitia ngazi za kisheria badala ya kuitafuta kupitia maandamano kama ilivyo kwenye maeneo mengine duniani.

Aidha Waziri Ndumbaro amewashukuru wasaidizi wa kisheria wa mkoa wa Kilimanjaro kwa namna ambavyo wanasaidia utoaji wa huduma za msaada wa kisheria kwa wahitaji  na hivyo kuwezesha wananchi kupata nafuu na haki inayohitajika kwa mujibu wa sheri.

“Nichukue fursa hii pia kuwapongeza wanasheria wote na taasisi zote zikiwemo zile za kibinafsi ambazo zitashiriki katika kutoa huduma wakati wote wa kampeni hii mkoani Kilimanjaro; huu ni Mkoa wa 17 tangu kuanza kwa kampeni hii, katika Mikoa 16 iliyopita wanasheria na taasisi mbalimbali wamefanyakazi nzuri, ni matumaini yetu kuwa kazi nzuri hizo zitaendelezwa hapa mkoani Kilimanjaro katika muda wote wa kampeni hii kama ulivyopangwa”, alisema.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Bw Nurdin Babu, alisema kampeni hiyo ni muhimu kwa wananchi, yenye faida kubwa  na kwamba imekuja wakati muafaka mkoani humo kutokana na ukweli kwamba watu wengi wana kiu na wengi wao hawana uwezo wa kugharamia huduma za kisheria.

“Sisi uongozi wa Mkoa tunaahidi kutoa ushirikiano wetu wa dhati katika kipindi chote cha kampeni hii; tunaahidi ya kuwa tutahakikisha ya kuwa huduma hizi zinafika hadi ngazi za chini kabisa za kiutawala ikiwemo ngazi ya vijiji ili kila mwananchi afaidi matunda yanayotokana na maono mazuri ya Rais Samia Suluhu Hassan na Serikali yake kwa ujumla”, alisema babu.

Naye Mkurugenzi wa taasisi ya ushauri wa kisheria mkoani Kilimanjaro ya KWIECO Wakili Elizabeth Minde, alimpongeza Rais Samia kwa kuja na wazo la kambi hiyo ya msaada wa kisheria.

“Kampeni hii imeakisi uwezo na maono chanya aliyonayo Rais Samia; itakuwa ya msaada mkubwa kwa wananchi wengi haswa wakiwemo wale ambao wako maeneo ya vijijini na ambao kwa sababu moja au nyingine hawakuwa na uwezo wa kulipia gharama kwa ajili ya kupata huduma za kisheria”, alisema.

Aliongeza kuwa “Nichukue fursa hii kumpongeza Rais na Serikali ya awamu ya sita kwa kuanzisha madawati ya msaada wa kisheria katika kila halmashauri jambo ambalo limewasogezea karibu huduma za kisheria wanachi wa ngazi zote na katika wilaya zote hapa nchini”.

Awali akiongeza Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Boniface Mwabukusi, ameisistiza jamii kuto puuza swala la kuandika wosia ili kuepusha changamoto zinazo jitokeza katika ugawaji mali.

“Kuna faida nyingi za kuandika wosia kwani mali zitagawanywa kulingana na maelekezo ambayo yaliachwa na marehemu na hivyo kuepusha ugomvi na mitafaruku mbalimbali ambayo ingetokea kutoka katika familia na ukoo mzima.”

“Changamoto kubwa zinazowagusa wananchi ziko kwenye ardhi na mirathi, ardhi inachangiwa na utafsiri mbaya wa sheria na upande wa mirathi ni kutokana na watu kutokupenda kuandika wosio,”alisema.



Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.