Wanufaika wa mikopo ya asilimia 10 Manispaa ya Moshi, wasisitizwa kuirejesha kwa wakati

MOSHI-KILIMANJARO

Wanufaika wa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri hapa nchini, wametakiwa kuhakikisha kwamba wanakuwa mfano mzuri, katika kurejesha fedha hizo kwa wakati ili watu wengine waweze kuendelea kukopa.

Mbunge wa Jimbo la Moshi Mjini Priscus Tarimo, ameyasema hayo, wakati akishuhudia Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Nurdin Babu akikabidhi hundi ya mfano yenye thamani ya Sh milioni 813.4 kwa vikundi vya 65 vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

Tarimo amewataka wale wote waliochukua mikopo hiyo kuirejesha kwa wakati ili kutoa fursa kwa vikundi vingine viweze kukopeshwa.

Aidha amewataka wajasiriamali hao kuwa mabalozi wazuri kwa kuwahamasisha watu wengine kujitokeza kwa wingi kuomba mikopo hiyo.

“Fedha za mikopo ya asilimia 10 zinazotolewa na halmashauri zinatokana na ukusanyaji wa mapato ya ndani ya halmashauri, hivyo amewasihi wafanyabishara kuhakikisha wanalipa kodi za serikali kwa usahihi pasipo kukwepa.”amesema Mbunge Tarimo.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi mikopo hiyo iliyofanyika katika viunga vya Manispaa ya Moshi mkoani humo, Mkurugenzi mtendaji wa  Manispaa hiyo Mwl. Mwajuma Nasombe, amesema tangu Rais Samia Suluhu Hassan, akamate wadhifa huo manispaa ya moshi imekwisha kutoa mikopo yenye thamani ya Sh bil. 2.5 hadi kufikia mwaka 2023.

Mwl. Nasombe amesema, baada ya kuwapatia mikopo  hiyo, wakazi wa Manispaa ya Moshi waliokidhi vigezo kwa mwaka huu, Wataalam wa Manispaa hiyo, wataanza kuwapatia elimu jinsi ya kuendesha miradi, utunzaji wa fedha, ujazaji wa mikataba na utunzaji wa kumbukumbu.

Hata hivyo Nansombe; amewataka waliokopeshwa kutorudia makosa ya awali yaliyofanya wakati fulani mikopo hiyo kusitishwa kutokana na wengine kushindwa kurudisha ambapo hadi sasa Manispaa hiyo inavidai vikundi kiasi cha Sh milioni 956.

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia halmashauri zake imekuwa ikitoa mikopo ya asilimia 10 kwa wananchi wake kama sehemu ya juhudi za kukuza maendeleo ya kiuchumi na kupunguza umaskini.
















Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.