Vyama vya siasa vyaombwa kuhamasisha wananchi, kushiriki zoezi la uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura

MOSHI-KILIMANJARO

Tume Huru ya Taifa ya uchaguzi, imewaomba viongozi wa vyama vya siasa mkoani Kilimanjaro, kuwahamasisha wanachama, wafuasi na mashabiki  wa vyama vyao, kujitokeza kwa wingi katika zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura  ambalo linatarajiwa kufanyika kwa siku saba kuanzia Desemba 11 hadi 17 mwaka huu.

Mkurugenzi wa Huduma za Kisheria Mtibora Seleman, ametoa wito huo, wakati wa uwasilishaji wa mada kuhusu maandalizi ya Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, kwa wadau wa uchaguzi mkoani Kilimanjaro.

Katika uwasilishaji wa mada yake hiyo Seleman, amewaomba viongozi wa vyama vya siasa kutumia  majukwaa na mitandao ya kijamii, kuwahamasisha wanachama wao kujitokeza kwa siku saba zilizotolewa na (INEC), kushiriki kikamilifu kwenye zoezi la uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura.

Amesema zoezi la uboreshaji wa Daftari la Wapiga Kura linawahusu wale wote ambao hajaandikishwa  katika daftari la wapiga kura na tayari wametimiza miaka 18 na wale ambao watatimiza miaka 18 katika siku ya uchaguzi mkuu mwaka 2025 na wale ambao wamepoteza kazi zao.

Aidha amesema kwenye mkoa wa Kilimanjaro Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi inatarajia kuandikisha wapiga kura wapya 180,540, ikiwa ni ongezeko la asilimia 18 ya wapiga kura 1,009726 waliopo kwenye daftari la kudumu la wapiga kura.

“Jumla ya asasi za kiraria 157 zimepewa fursa ya kutoa elimu ya mpiga kura katika zoezi la uboreshaji wa daftari la wapiga kura,” na kuongeza kuwa utaratibu wa wafungwa, INEC imefanya maboresho katika uandikishaji kwa kutoa fursa kwa wafungwa waliofungwa chini ya miezi sita na mahabusu ambao hawajahukumiwa kuzshiriki katika zoezi la uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura,”amesema.

Kwa upande wake  Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Balozi Omar Ramadhan Mapuri, amewataka wadau ambao wameshiriki katika mkutamno huo kuwa mabalozi wazuri kwa wengine ambao hawakupata nafasi ya kushiriki katika mkutano huo.

Mkutano wa Tume na Wadau wa Uchaguzi kuhusu Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga kura, umewakutanisha wadau mbalimbali  wa uchaguzi vikiwemo vyama vya siasa, asasi za kirari, wahariri wa vyombo vya habari, watu wenye ulemavu, viongozi wa dini, vikosi vya usalama, vijana na viongozi wa kimila.
















Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.