Wakristo nchini watakiwa kutafakari kuzaliwa kwa Yesu Kristo

KILEO-MWANGA.

Wakristo nchini wametakiwa kutafakari mahusiano yao na Mungu, kisha kukabidhi maisha yao kwa Yesu Kristo aliyebeba amani ya kudumu ndani ya maisha yao.

Akihubiri Desemba 22,2024 katika ibada ya kusimikwa kwa mchungaji  wa Kanisa la Africa Mission Evangelism Church Tanzania (AMEC), Parokia ya Kileo, Wilayani Mwanga, mkoani Kilimanjaro;

Katibu wa Theolojia Mchg. Yuda Kundael Pallangyo, Jimbo la Arusha, amesema Wakristo, waliopata neema ya kusherehekea Sikukuu ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo, ni muhimu kujua kwamba Mungu, amejifunua katika maisha yao na kwa kutafakari hilo, amewataka kukabidhi maisha yao kwa Yesu Kristo, aliyebeba amani ya kudumu ikiwa na majibu ya changamoto zao.

Akinukuu maandiko katika Biblia takatifu, Mchg. Pallangyo, amesema ujio wa Yesu Kristo, ulitabiriwa na manabii kabla ya kuzaliwa kwa mwanadamu aliyefanya miujiza mikubwa, akauwawa kabla ya kufufuka na kupaa mbinguni, baada ya maisha ya miaka 33 duniani, hivyo kifo chake ndio msingi wa ahadi ya Mungu kuunganisha upya, mahusiano yake na mwanadamu kwa ajili ya kumwagika damu.

Aidha Mchg. Huyo, amewasihi Wakristo hasa wale wanaopitia changamoto na hali ngumu, kuwa na subri na imani na kuwasihi kutokukata tamaa pindi wanapokuwa wakipitia changamoto mbalimbali za maisha.

Mchg. Pallangyo, amesema wakati wa Mungu unapofika huwainua watu kutoka chini na kuwapa baraka na mafanikio, licha ya changamoto na hali ngumu za maisha wanazozipitia kwani Mungu ana njia ya kuwainua na kuwapa neema wakati wake.

Aidha amesema  mbele ya uso wa Mungu hakuna kudhaurika na kwamba mtu ambae anakuona ni wa chini, Mungu anakwenda kumwinua na kuwa mtu wa viwango vingine huku akitolea mfano katika mji wa Nazareth ambao ulikuwa unaonekana hauwezi kutoa mtu mashuhuri, lakini alikuja kutokea mtu ambaye ni mwana wa Mungu nae ni Yesu Kristo.

“Wako baadhi ya watu wanasema inawezekanaje watu wa Parokia ya Kileo wakapata mchungaji, wako watu wa Jimbo la Kilimanjaro watasema inawezekanaje Kanisa la AMEC lenye waumini wachache kiasi hiki likatoa mchungaji? Nataka nikwambie…Bwana ana mpango wa kuliinua kanisa lake na anapoliinua kanisa lake analiinua kutoka katika eneo ambalo huwezi kutarajia, kama ilivyokuwa kwenye mji wa Nazereth uliokuwa ukidhaurika lakini Masihi ndipo alipotokea pale.

Kwa upande wake Askofu Mkuu wa Kanisa la Furaha Tanzania, Jones Mola, amewasihi waumini kuwajibika kwa wachungaji wao kwa kuwatembelea na kuwatunza, huku akisisitiza umuhimu wa mshikamano na msaada wa viongozi wa kiroho.

Askofu Mola aliweka wazi kwamba wachungaji ni vionyesho vya huduma ya Mungu kwa watu, na ni jukumu la waumini kuwasaidia ili waweze kutimiza majukumu yao kwa ufanisi.

Aidha Askofu Mola  amewasihi wakristo waliojiunga na kanisa la AMEC, wasikubali kurudi nyuma, kwani wako baadhi ya watu watakuja na kuwalaghai kwamba kujiunga na kanisa hilo watakuwa wamepotea na hivyo kukatishwa tamaa.

Katika ibada hiyo Askofu Mkuu wa Kanisa la Africa Mission Evangelism Church Tanzania (AMEC) Baltazari Kaaya, alimsimika Mchungaji Pauli Mark Assey, kuwa Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la AMEC Parokia ya Kileo.


















Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.