Shemasi ' Pauli Marki Assey' kusimikwa daraja la uchungaji Desemba 22, mwaka huu

Askofu Mkuu wa Kanisa la Furaha Tanzania na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT),  akisalimiana na Shemasi Pauli Marki Assey, alipotembelea ofisi hiyo Desemba 6,2024

MOSHI-KILIMANJARO

Askofu Mkuu wa Kanisa la Furaha Tanzania, Jones Mola, amewataka wachungaji wanaoingizwa katika huduma ya Mungu, kuonyesha uaminifu na kujitolea kwa dhati.

Hayo ameyasema Desemba 7, 2024, mjini Moshi,  alipokuwa akiongea na waandishi wa habari,  akiwahimiza wachungaji kuwa na uaminifu na moyo wa kujitolea katika kazi yao ya kumtumikia Mungu, huku akisema kwamba watumishi wa Mungu wanapaswa kumwangalia Mungu kwanza na si watu, kwani wengi hawakuwa na fursa ya kumwona lakini walichagua kumtumikia.

Akinukuu kitabu cha Injili ya Yohana 12: 26 Askofu Mola amesema “Mtu ye yote anayetaka kunitumikia lazima anifuate; ili mtumishi wangu awepo mahali nilipo; na mtu ye yote akinitumikia, Baba yangu atampa tuzo ya heshima.

Aidha Askofu Mola, amempongeza Shemasi Pauli  Marki Assey, anayetarajiwa kupandishwa daraja la uchungaji hivi karibuni, kwa kazi hiyo ambayo  Mungu amemuitia, atakiwa kutambua kwamba  Mungu ameacha watu wengi sana ambao hakuwaona na kumuona yeye, ni vizuri akaenda kuonesha uaminifu na moyo wa kumpenda Mungu na asiangalie watu bali amwangalie Mungu, amuongoze na roho mtakatifu kuitenda kazi yake, alipende kanisa, nchi na viongozi wake.

Kwa upande wake Mchungaji wa Kanisa la Africa Mission Evangelism Church Tanzania Parokia ya Mamba (AMEC), ambaye pia ni Msaidizi wa Mkuu wa Jimbo la Kilimanjaro Davis Makundi, amesema wanalo tukio la kiimani la kumsimika, Shemasi Paulo  Marki Assey kuwa mchungaji  wa Kanisa la AMEC Kata ya Kileo, tukio ambalo litafanyika Desemba 22 mwaka huu, kwenye kata hiyo, Wilaya ya Mwanga, mkoani humo.

Mchungaji Makundi amesema tukio hilo, litatanguliwa na ibada ya kawaida na baada ya hapo kutakuwa na tendo la kumsimika Assey kuwa mchungaji, sambamba na tukio la kuwapokea wakristo watakaojiunga na kanisa la AMEC.

Amesema katika tukio hilo Askofu Mkuu wa Kanisa la Africa Mission Evangelism Church Tanzania kutoka Makao Makuu Jijini Arusha, Baltazari Kaaya, ndie atakaye msimika daraja la uchungaji, huku viongozi mbalimbali  wa kidini na kiserikali watakuwepo kushiriki ibada hiyo.

Aidha amesema kama kanisa wanauhitaji mkubwa wa watumishi wa Mungu watakao hudumu katika shamba la Bwana, hivyo kusimikwa kwa mchungaji huo atakwenda kuleta hamasa kubwa ya kuwahudumia wakristo wa kata ya Kileo waliokuwa wamekosa huduma hiyo kwa kipindi kirefu.

Naye Shemasi Pauli Marki Assey, amesema tangu akiwa kijana mdogo, alikuwa na wito wa kumtumikia Mungu, kwa hatua ambayo amefikia ya kusimika kwenda kuwa mchungaji  ni Mungu amesikia hitaji lake la Moyo wake la kwenda kuihubiri injili kwa mataifa yote.

Viongozi watakaoshiriki tukio la kusimikwa mchungaji huyo mteule ni pamoja na Msaidizi wa Askofu Mchg. William Ayo, Mkuu wa Jimbo la Arusha Mchg. Elidaima Mushi, Katibu wa Theolojia Mchg. Yuda Pallangyo, Askofu Mkuu wa Kanisa la Furaha Tanzania Jones Mola, Mkuu wa Jimbo la Kilimanjaro Mchg. Willison Kawiche.

Pia viongozi wa Serikali walioalikwa ni pamoja na Mbunge wa Jimbo la Mwanga Joseph Tadayo, Mkuu wa Wilaya ya Mwanga Mwahamisi Munkunda, Mkuu wa Polisi Wilaya ya Mwanga na Seikh wa Wilaya ya Mwanga, ambapo pia kutakuwepo na Kwaya ya AMEC kutoka Msitu wa Tembo Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara, pamoja  na kwaya kutoka Jimbo la Arusha.






Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.