MUWSA kukusanya Sh bilioni 10 mwaka 2024/2025


MOSHI-KILIMANJARO.

Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Moshi (MUWSA), imepanga kukusanya na kutumia jumla ya Sh bilioni 10 kwa mwaka 2024/2025 lengo likiwa ni kuimarisha upatikanaji wa huduma za maji kwa wananchi wanaowahudumia.

Mkurugenzi mtendaji wa (MUWSA) Mhandisi Kija Limbe, ameyasema hayo desemba 17, 2024 wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa bajeti kwa mwaka 2024/2025 kwenye Kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC), na kusema kuwa  Mamlaka hiyo imeweka vipaumbele ambavyo vitazingatiwa katika mpango huo, ili kufikia lengo la upatikanaji wa huduma ya majisafi na salama kwa wananchi wote.

Amesema MUWSA imepanga kukusanya na kutumia jumla ya Sh bilioni 10, kati ya fedha hizo Sh bilioni 3.5 ni fedha kutoka Serikali Kuu, Sh bilioni 1, mkopo kutoka Mfuko wa Taifa wa Maji, Sh bilioni 1.2, fedha za ufadhili kutoka KFW huku Sh bilioni 4.2 kutoka kwenye Mapato ya ndani ya Mamlaka kwa ajili ya uwekezaji.

Amesema, kupitia mapato yake ya ndani Mamlaka hiyo, pia imefanikiwa kusimamia na kukamilisha utekelezaji wa mradi mpya wa Majisafi na ujenzi wa chanzo cha Karanga Darajani, ambapo wananchi wa kata za Pasua, Bomambuzi, na Mabogini, wameanza kunufaika na huduma ya upatikanaji wa Majisafi na salama.

Mhandisi Limbe, amesema kwa kutumia mapato ya ndani, Mamlaka hiyo imefanikiwa kuongeza mtandao mpya wa usambazaji wa Majisafi kwa kilomita 104.395, kuongeza mtandao wa majitaka kilomita 7.4 pamoja na kufanya ukarabati wa  mtandao chakavu kwa zaidi ya kilomita 23.21, kuunga jumla ya wateja wapya 4,308 kwenye huduma ya Majisafi huku wateja wapya 47 wameungwa kwenye mtandao wa majitaka.

Vilevile amesema Mamlaka hiyo, imefanikiwa kuongeza kiwango cha ukusanyaji wa mapato kwa mwezi, kutoa wastani wa Sh bilioni 1.1 hadi kufikia makusanyo kwa mwezi wastabni wa Sh bilioni 1.3

Mbunge wa viti maalum mkoa wa Kilimanjaro Shally Raymond, alimpongeza Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Moshi Kija Limbe, kwa jitihada kubwa anazozifanya za kuhakikisha upatikanaji wa huduma ya majisafi na salama kwa wananchi zinapatikana kwa muda wote.

Naye Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Vunjo Gulatone Masiga, ametoa ushauri kwa Mamalaka ya Maji MUWSA kuendelea, kutoa elimu kwa umma kuhusiana na matumizi sahihi ya maji na namna bora ya kutunza na kulinda miundombinu ya maji kwa huduma endelevu sambamba na kutafuta vyanzo vya maji mbadala ili kuongeza wigo wa upatikanaji wa maji.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Nurdin Babu, amemuagiza mkugugenzi wa Mamlaka ya Maji (MUWSA), kuanza kutekeleza ufungaji wa Pre-paid meter (Mita ya Malipo ya kabla) kwa taasisi za umma kama ilivyo kwa LUKU kwenye (Umeme).






Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.