Mangi Gilbert Shangali kusimikwa Desemba 14,2024

Mangi mkuu wa Machame Gilbert Shangali, anatarajiwa kusimikwa Desemba 14,2024

MOSHI-KILIMANJARO.

Mkuu wa Mkoa wa Kiliamnajro Nurdin Babi, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika tukio la kusimikwa kwa Mangi mkuu wa Machame Gilbert Shangali, litakalofanyika Desemba 14, mwaka huu, kijiji cha Machame Wari, Wilaya ya Hai mkoani humo.

Hayo yamesemwa Desemba 9,2024 na Mwenyekiti wa Kamati ya maandalizi, Clement Andrea Shangali, wakati akizungumza na waandishi wa habari mjini Moshi, ambapo amesema kuwa, ni sehemu ya kuendeleza mila na desturi za Wachaggawa eneo la Machame.

Aidha Mwenyekiti huyo wa kamati ya maandalizi Clement Andrea Shangali, amesema maandalizi ya kumsimika Mangi Gilbert SHangali, yameshakamilika, ambapo Mwenyekiti Mstaafu wa Umoja wa Machifu Tanzania (UMT) Frank Mareallle, atafanya shughuli hiyo ya kumsimika kimila, ambapo tukio  hilo litaanza majira ya saa tatu asubuhi, huku akitoa wito kwa wananchi kuhudhuria kwa wingi kushuhudia tukio la kusimikwa kwa Mangi mpya wa Machame.

Amesema katika tukio hilo pia kutakuwepo na machifu wengine kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara na Visiwani, Wabunge, Madiwani, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania mkoa wa Kilimanjaro (JMT) Jones Mola, Mkuu wa Wilaya ya Moshi James Kaji, pamoja na viongozi wa madhehebu ya kidini.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa ukoo Dk. Harold Shangali, amesema kuteuliwa kwa Gilbert Shangali, kuwa Mangi wa Wana Machame, anayo nafasi kuwa ya kuhakikisha kwamba  anakwenda kusimamia maadili ambayo kwa kiasi kikubwa yameporomoka katika jamii.

Aidha Dk. Shangali, amesema machifu wana mchango mkubwa katika kulinda maadili na kutatua changamoto za kimaadili katika jamii licha ya kuwa yanashughulikiwa katika ngazi ya serikali.

Naye Katibu wa Umoja wa Machifu mkoa wa Kilimanjaro Joseph Mselle, amesema Afrika ilikuwa na mfumo wake wa utawala, uliokuwa unarithishwa kizazi kimoja hadi kizazi kingine.

Akizungumzia tawala za jadi katika nchi ya Tanzania Mselle; amesema ni alama ya mfumo wa kiuongozi kwa Waafrika kabla ya ukoloni kitu ambacho ndicho kilikuwa ni kielelezo cha kutambulisha tamaduni zetu.

Naye Mangi mteule wa Machame Gilbert Shangali, amewashukuru wananchi wa machame, kwa kuona anafaa na hivyo kumpa heshima hiyo, ambayo inamfanya kuwa mmoja wa viongozi wa kimila katika himaya hiyo.

Chifu mteule Gilbert Gilead Shangali ni mtoto wa Kwanza kuzaliwa kwa Mangi (Gilead Abdiel Shangali) na ni Mjukuu wa Mwitori Abdeil Shangali na ni Kitukuu cha  Mangi Shangali Ndeserua.

Chifu mteule Gilbert Shangali, alizaliwa Machame mwaka 1973,baadaye alijiunga na masomo ya shule ya msingi  Machame kuanzia mwaka 1980 hadi 1987.  Shule ya sekondari (O-Level) Mwaka 1988 hadi 1992, na shule ya sekondari ya Siha (A-Level) mwaka   1993 hadi 1995.

Baada ya kumaliza masomo ya sekondari, alijiunga na Chuo cha Oshwal Nairobi nchini Kenya, kuanzia mwaka 1996 hadi 1999. Ambapo alihitimu masomo yake na kuwa na Taaluma ya Uongozi na Utawala.

Mwenyekiti wa ukoo Dk. Harold Shangali wa kwanza (kushoto), Mwenyekiti wa Kamati ya maandalizi, Clement Andrea Shangali (katikati) na Katibu wa Umoja wa Machifu mkoa wa Kilimanjaro Joseph Mselle, wakiwa katika kikao cha maandalizi ya sherehe za kusimikwa mangi mkuu wa Machame Gilbert Shangali.

Machifu kutoka mikoa mbalimbali Tanzania bara na Visiwani kushiri tukio la kusimikwa kwa Mangi wa 52 wa Machame, tukio litakalofanyika kijiji cha Machame Wari , wilaya ya Hai, mkoani Kilimanjaro.

                                      Mwenyekiti wa ukoo Dk. Harold Shangali 

Mwenyekiti wa Kamati ya maandalizi ya sherehe za kusimikwa kwa Mangi mkuu wa Machame Gilbert Shangali. Clement Andrea Shangali.


Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.