Mabaraza ya Wafanyakazi yatumike Kujenga demokrasia mahala pa za kazi

MOSHI-KILIMANJARO.

Mabaraza ya wafanyakazi, yametakiwa kutumika kama chombo muhimu katika kuboresha na kuimarisha demokrasia kwenye eneo la kazi, badala ya kutumika pekee kukusanya na kupitia maoni ya watumishi.

Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi, Idara ya Uhamiaji Taifa (TUGHE) Joel George Kaminyoge, aliyasema hayo Desemba 10,2024, wakati wa ufunguzi wa Baraza la Wafanyakazi, Idara ya Uhamiaji, mkutano uliofanyika katika ukumbi wa Chuo cha Uhamiaji cha Kikanda (TRITA) Moshi mkoani Kilimanjaro.

Amesema kuwa mabaraza hayo yanahusisha ushirikishwaji wa wafanyakazi katika maamuzi ya taasisi au shirika wanamofanyia kazi, jambo ambalo huongeza uwazi, ufanisi  na uwajibikaji mahala pa kazi.

“Zamani mabaraza haya ya wanyakazi yalikuwa ya kiharakati sana, na ndio maana kulikuwa na migogoro mingi kati ya wafanyakazi na waajiri ambayo, ilikuwa haiishi,  lakini kwa sasa hivi sivyo, kwa sababu tunakaa kwenye meza moja na kukubaliana kati ya waajiri na wafanyakazi na hivyo kumekuwepo kwa mafanikio makubwa zaidi, ukilinganisha na huko tulikuwa zamani.”amesema Kaminyoge.

Aidha amewataka watumishi wa umma, kuhakikisha kwamba wanapunguza, kutumia simu janja wanapokuwa kazini ili waweze kutoa huduma bora kwa wananchi nchini.

Amesema kumekuwa na malalamiko mengi kwa wahudumu kwa baadhi ya taasisi za serikali kushindwa kuwahudumia wananchi vizuri kutokana na matumizi yaliyopitiliza ya simu janja.

“Masuala ya kutumia muda mwingi kuchati kwenye simu, sisi kama Tughe tunasema hapana, wanachama wetu wanatakiwa kuwajibika, ili kuongeza tija, ukiwa unahitaji kulipwa vizuri mshahara wako, utahitaji kulipwa vizuri baada ya  kufanya kazi kwa bidii na hivyo kuongeza pato,”amesema.

Mbali na hilo Kaminyonge amesema wakati ambao Tughe  inaadhimisha miaka 30 tangu kuanzishwa kwake mnamo mwaka 1994 imepitia mabadiliko mengi ambayo yamekuwa na tija ikiwemo ujenzi wa watumishi mahali pa kazi.

“Miaka 30 ya Tughe kwangu mimi ni mafanikio makubwa na miongoni mwa hayo, ni kuwepo kwa mabaraza mawili ya wafanyakazi mahali pa kazi, ndio yanayowezesha kuwakutanisha kwa pamoja kati ya waajiri na wafanyakazi, kukaa pamoja, kupanga mipango ya taasisi lakini pia kuongeza mshikamano na ufanisi mahala pa kazi na ndio maana huwezi kusikia kuna migogoro katika eneo letu,”amesema.

Kwa upande Kaimu Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi Idara ya Uhamiaji Kamishna Gerald Kihinga, amesema wakati Tughe  inaadhimisha miaka 30 tangu kuanzishwa kwake, yako mafanikio makubwa ambayo inajivumia kwa kipindi chote hicho ikiwemo ukamilishaji wa majengo yaliyokuwa hayajakamilika, pamoja na ufungaji wa mifumo.

Aidha katika Kikao hicho kilichowakutanisha wanachama wa TUGHE, Idara ya Uhamiaji kote nchini katika kujadili Bajeti ya Idara ya Uhamiaji kwa mwaka wa fedha 2024/25 wamekumbushwa kuhusu kuendelea kujikinga na maradhi yanayoambukizwa kwa kujamiiana ili kuijenga Tanzania ni lazima watumishi wawe na afya njema.

Sheria ya Ajira na Mahusiano ya Kazi 2004 na Sheria ya Taasisi za Kazi 2004  zinatoa haki kwa wafanyakazi wote kujiunga na vyama vya wafanyakazi na kwa waajiri kuunda vyama vya waajiri kwa maslahi mapana ya ujenzi wa nchi.










Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.