Naibu Waziri wa Afya Dkt.
Godwin Mollel, ameahidi kuisaidia shule ya sekondari ya New Dawn, iliyoko
Wilaya ya Same, kwa kutoa msaada wa Kompyuta 40 na mashine ya kudurufia
(Photocopy), ili kuifanya shule hiyo kuendelea kuwa shule bora zaidi.
Dkt. Mollel, ameahidi kutoa
msaada wa vifaa hivyo Novemba 30,2024, wakati wa hotuba yake ambayo aliitumia
pia kujibu chanagamoto zilizotajwa katika risala iliyosomwa na mwakilishi wa
wanafunzi, wakati wa hafla ya tatu ya kidato cha nne, ambapo pamoja na mambo
mengine wamesema shule inakabiliwa na ukosefu wa kompyuta na mashine ya kurudufia
(Photocopy), ukosefu wa uzio, maji safi na salama pamoja na maktaba.
Kuhusu suala la changamoto
ya maji safi na salama shuleni hapo Dkt. Mollel
amesema atawasiliana na Waziri wa Maji Jumaa Aweso, ili aweze kuona
tatizo lililopo katika shule hiyo ambayo inalea watoto hasa wanaotoka katika
familia zenye vipato duni na yatima, waweze kusaidiwa kupata maji karibu na eneo lao la shule.
Kwa upande wake Mkurugenzi
Mkazi wa Shirika la New Dawn Community Internation
Dkt. Stephano Mshomi, amesema shule hiyo
imeanzishwa kwa lengo la kuwahudumia wanafunzi wanaotoka katika familia zisizo
na uwezo kutimiza ndoto zao.
Dkt. Mshomi, amesema
taasisi ya New Dawn Community international ni daraja ambalo wanafunzi wataweza
kupata elimu hadi kufikia ngazi ya vyuo na vyuo vikuu ili waweze kutimiza ndoto
walizojiwekea.
Awali akizungumza Mkuu wa
shule ya Sekondari ya New Dawn Emmanuel Kitadu, amesema shule hiyo, imekuwa
ikifanya vizuri katika eneo la taaluma, kwani mpaka sasa shule hiyo ni miongoni
mwa shule 10 bora inayofanya vizuri katika Wilaya ya Same, mkoani humo.
Ameongeza kuwa katika mtihani
wa kidato cha nne mwaka 2022 shule ilishika nafasi ya 10 kiwilaya na mwaka 2023 shule hiyo ilishika nafasi ya 9
kati ya shule 57 zilizopo wilayani humo na kwamba kwenye eneo la michezo shule hiyo
pia imekuwa ikishiriki vyema mashindano ya michezo mbalimbali ya kiwilaya,
kimkoa na kitaifa.
Mwl. Kitadu, amesema kuwa
licha ya kuwa na ufaulu mzuri, bado shule hiyo inakabiliwa na changamoto
mbalimbali ikiwemo ya uhaba wa vifaa vya kujifunzia na kufundishia, maktaba na
chumba cha kompyuta.
Akisoma risala kwa niaba ya
wahitimu wa kidato cha Nne, Rais wa Serikali ya wanafunzi Sebastian Christopher,
amesema kwa miaka minne waliyokuwepo shule hapo, wamepata elimu bora ya
darasani, iliyowajengea misingi bora ya kitaaluma ambayo itawawezesha kuendelea
na elimu ya juu ili kutimiza ndoto zao.
Pia amesema wakiwa shuleni
hapo, hawakuishia tu, kujifunza mambo ya kitaaluma darasani, bali walijifunza, kufanya
shughuli mbalimbali za mikono ikiwemo kilimo, ufugaji na michezo, mambo ambayo
amesema yatawasaidia kuepuka kwa wategemezi kwani wamejifunza kuwa wabunifu.
Shule ya New Dawn ilianza rasmi kidato cha kwanza mwaka 2019, ikiwa na jumla ya wanafunzi 36, ambapo shule hiyo, hutoa elimu kwa wanafunzi wa kike na kiume kwa kusimamia misingi ya nguzo kuu tano, ambazo ni makuzi ya kiroho, kitaaluma, kitabia, ujuzi na ufundi na huduma za kijamii.