Tadayo; kutumia tamasha la Mwanga festival kutembelea jiwe la ambalo watoto waliokuwa wakizaliwa na changamoto ya ulemavu kwenda kutupwa “Mkumbavana”

Jiwe la "Mkumbavana" jiwe ambalo watoto waliokuwa wakizaliwa na changamoto ya ulemavu, wazazi wao walikuwa wakiwapeleka na kuwatupa na kufia huko ili kuondoa laana na mikosi katika familia zao.

MWANGA-KILIMANJARO.

Mbunge wa Jimbo la Mwanga Joseph Anania Tadayo, anatarajia kutumia fursa ya kiutalii kupitia Tamasha la Mwanga Festival and Marathon 2024, kutembelea vivutio vya utalii vilivyomo katika jimbo hilo kwa lengo la kuhamasisha wananchi kushiriki tamasha hilo litakalofanyika Desemba 27 mwaka huu.

Moja ya kivutio kikubwa ambacho anatarajia kukitembelea Mbunge Tadayo ni pamoja na jiwe “Mkumbavana” jiwe ambalo watoto waliokuwa wakizaliwa na changamoto ya ulemavu, wazazi wao walikuwa wakiwapeleka na kuwatupa na kufia huko ili kuondoa laana na mikosi katika familia zao, na Wajerumani walipokuja katika wilaya hiyo waliwaelimisha wananchi hao na kuacha tabia hiyo.

Akizungumza na Jukwaa la Mwanga Festiva and Marathon Tadayo, amewakumbusha wananchi wa Mwanga kujenga utamaduni wa kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo katika wilaya hiyo, ikiwa ni sehemu ya kukuza maarifa, ujuzi, afya ya akili na kuongeza pato la taifa.

“Wilaya ya Mwanga ni miongoni mwa maeneo yaliyo na utajiri  mkubwa wa vivutio vya utalii ambavyo bado vinahitaji kutembelewa na kutengenezewa simulizi  zinazohitaji  kuwafikia watu wengi zaidi ikiwemo ya mtunzi asilia wa wimbo wa maarufu wa kizalendo wa Tanzania, Tanzania, Nakupenda kwa moyo wote, ambaye anatoka wilaya ya Mwanga Kata ya Kifula.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Mwanga Mwanahamisi Munkunda, amesema suala la uwekezaji kwenye vivutio hivyo bado ni fursa nyingine iliyo wazi kwa watu walio na nia pasipo kujali ni wazawa au wageni.

DC Munkunda anazitaja fursa za uwekezaji zilizopo katika sekta ya utalii kuwa ni pamoja na ujenzi wa nyumba za kulala wageni, hoteli, kambi za watalii  katika Bwawa la Nyumba ya Mungu na  Ziwa Jipe, huku akisema kuwa bado zipo fursa nyingi za uwekezaji katika wilaya ya Mwanga na kinachohitajika ni maamuzi na uthubutu wa wahitaji wenyewe.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya maandalizi ya Mwanga Festival an Marathon Frida Mberesero, amesema kupitia tamasha hilo wadau mbalimbali wameendelea kuhamasishwa kuja kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo  wilayani humo.

Mratibu wa Tamasha hilo Zawadi Mirambo, amesema Wilaya ya Mwanga kwa kushirikiana na wadu wa utalii ikiwemo kampuni ya Utalii ya Kisangara Tours Ltd, wameandaa tamasha maalumu la kukuza utalii, zikiwemo mbio kilometa 5, 10, na 21 huku Kauli mbiu  ikiwa ni Mwanga Yetu, Utalii Wetu.

“Mbio hizi zitafanyika Desemba 27 mwaka huu kuanzia saa kumi na mbili asubuhi, ambapo mbio za Km 5, hadi barabara ya Lang’ata, mbio za Km 10 zikianzia uwanja wa Cleopa Msuya hadi Standi ya reli Kisangiro huku mbio za Km 21 zikianzia uwanja wa Cleopa Msuya hadi Kisangiro.

Ameongeza kuwa washiriki wa mbio hizo watapata T-shert pamoja na medali na baada ya ya mbio hizo kutamatika, itafuatiwa na  Tamasha la Utalii litakalofanyika katika ufukwe wa Nyumba ya Mungu, ambapo kutawakuwa na nyama choma, vyakula vya asili, ngoma  za Wapare na jamii ya kifugaji ya Ki-maasai.

Amefafanua kuwa siku ya Desemba 28 mwaka huu kutakuwa na safari ya kwenda kutembelea Hifadhi ya Taifa Mkomazi, kwa wale watakoshiriki ziara hiyo watatakiwa  kujiandikisha kwa kupitia namba ya simu ya 0755-002 886.

Amesema watu watakaopata fursa ya kutembelea hifadhi ya Mkomazi  wataweza kuwaona Faru weusi, kwa ukaribu zaidi tofauti na hifadhi zingine ambazo unaweza kutembelea, Mbwa mwitu, Tembo, Twiga, Nyati na ndege wa aina tofauti.




Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.