Moto wateketeza hekta 60 za misitu ya Kamwala, Kindoroko, Mramba

MWANGA-KILIMANJARO.

Jumla ya hekta 60 za misitu zilizoko katika hifadhi ya misitu ya Kamwala One, Kindoroko, Kamwala two na Mramba zilizoko Wilaya ya Mwanga, mkoani Kilimanjaro, zimeteketea kwa moto kwa mwaka huu, kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo shughuli za kibinadamu.

Mhifadhi Daraja la Pili kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Wilayani humo Pius Clement Maganga, ameyasema hayo Novemba 13,2024 wakati akizungumza na Waandishi wa habari wilayani humo.

Amesema uharibifu uliofanywa na mioto hiyo, uliathiri mpaka huduma za kijamii ikiwemo huduma za maji, baada ya miundombinu ya usambazaji maji iliyokuwa inatoa maji ndani ya  misitu hiyo kuungua kwa moto na kusababisha wananchi kukosa huduma hiyo.

“Kwa tathmini ya haraka tuliyoifanya tukijumuisha misitu yote iliyoteketea mwaka huu, takribani hekta 60 ziliteketea kwa moto”, amesema Maganga.

Ameendelea kusema kuwa changamoto hiyo hutokea haswa nyakati za kiangazi ambapo wananchi wanapokuwa katika kutayarisha mashamba yao kwa ajili ya shughuli za kilimo, ambapo huwasha moto kwa ajili ya kuchoma majani yaliyoko shambani.

Amesema changamoto nyingine ni ile ya wachungi kupeleka mifugo yao kwenye misitu kwa ajili ya malisho ya mifugo yao kutokana na ukame wakati wa kiangazi.

“Hali hii imeleta athari kubwa ikiwemo kwenye sekta ya utalii kutokana na misitu kuharibiwa vibaya; wito wangu kwa wananchi waepuka tabia hizi za uharibifu ili misitu iwe salama na hivyo kuchangia uchumi wa Taifa kupitia utalii wa ikolojia”, amesema.

Ameongeza kuwa “Ni vyema watu wakajenga tabia ya kuwa na uzalendo na kuepuka shughuli ambazo zitaathiri misitu kwa vile madhara hayatakuwa kwa misitu, wanyama na mimea tu bali hata kwa wananchi wanaoishi kuzunguka  misitu hiyo”, amesema Maganga.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.