Meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), Mkoa wa Kilimanjaro Injinia Weransari Munisi wa kwanza kulia aliye vaa koti jeusi akisaini kandarasi ya ujenzi wa mradi wa maji kata ya kihurio wenye thamani ya Sh bilioni 4.1 wa tatu kutoka kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Same Kasilida Mgeni akishuhudia utiaji wa saini hizo.
SAME-KILIMANJARO.
Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), Mkoa
wa Kilimanjaro, umesaini kandarasi ya ujenzi wa mradi wa maji katika kata ya
Kihurio jimbo la Same Mashariki mkoani humo, na Kampuni ya Fesam Construction
Limited yenye makao makuu yake Jijini Dar es Salaam ambayo itatekeleza mradi
huo kwa miaka miwili.
Meneja wa RUWASA mkoa wa
Kilimanjaro Injinia Weransari Munisi, ameyasema hayo jana, mara baada ya kusaini kandarasi hiyo katika
ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya same, na kampuni ya Fesam Construction Limited.
Amesema mradi ambao wananchi
walikuwa wakiutumia ulijengwa kwa miaka ya 1970, ulijengwa wakati huo idadi ya
watu walikuwa wachache, kwa sasa hivi idadi ya watu imeongezeka zaidi ya mara
10 hali ambayo ilikuwa ni changamoto ya upatikanaji wa huduma ya maji.
Injinia Munisi, amesema, ili
kuondoa adha hiyo ya kuendelea kukarabati kila mwaka, serikali imeleta mradi
mpya wa maji na kwamba kwa mwaka wa fedha 2024/2025 kiasi cha Sh Bilioni 4,178, 753, 349 zitakwenda
kutumika kwa ajili ya ujenzi wa mradi mpya wa maji.
Akisoma taarifa ya utekelezaji
wa mradi huo Meneja wa (RUWASA), Wilaya ya Same Injinia Abdallah Gendaeka, amesema mradi huo
utahudumia kata nzima ya Kihurio yenye vijiji vitatu vya Kakonkolo, Kongei na
Uzambala vyenye wakazi 10,249 sawa na asilimia 3.9 ya wakazi waishio vijijini.
Amesema mradi huo utatekelezwa
kwa muda wa miaka miwili kuanzia tarehe desemba 2024 hadi desemba 2026 na
kwamba utahusisha ujenzi wa miundombinu mipya, ikiwemo ujenzi wa dakio la maji
kutoka mto Sesemi, ulazaji wa mabomba yenye urefu wa kilometa 54.9 , ujenzi wa
tangi kubwa lenye lita 500,000, vituo 51 vya kuchotea maji na vivunja nguvu
(presha) pamoja na ukarabati wa matangi yaliyopo.
Mkuu wa Wilaya ya Same Kasilda
Mgeni, amemtaka mkandarasi huyo kujenga mradi huo kwa kuzingatia ubora
unaotakiwa, sanjari na kuzingatia muda wa kukamilisha mradi huo ili wananchi
waanze kupata huduma ya maji hususan katika maeneo ya kutolea huduma za
kijamii.
Aidha mkuu huyo wa Wilaya amewataka
wananchi wa Kihurio kuhakikisha wanatoa ushirikiano kwa mkandarasi kwenye
kipindi chote cha utekelezaji wa mradi, ikiwa ni pamoja na kuwa walinzi wa
kwanza wa mitambo itakayotumiwa na wakandarasi kutekeleza mradi huo.
Akizungumza kwa niaba ya
wananchi wa kata hiyo, mkazi wa Kihurio Aza
Sadick Mashambo, ameishukuru Serikali kwa kuwapatia mradi huo ambao utakwenda
kuwaondolea adha ya maji ambayo walikuwa wakiipata kwa kioindi kirefu.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa
kampuni ya Kampuni ya Fesam Construction Limited Injinia Charles Maganga, ameahidi
kuifanya kazi hiyo kwa wakati kulingana na mkataba unavyomtaka ili mradi huo, uweze
kutoa huduma kwa wananchi kama ilivyokusudiwa na Serikali.
Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na
Makazi ya mwaka 2022 Kata ya Kihurio ina jumla ya wakazi 10,249, imekuwa
ikikabiliwa na ukosefu wa maji safi na salama hali inayowalazimu wakazi hao
kutembea umbali mrefu kutafuta huduma hiyo.