Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia, Tamisemi zaelekezwa kuharakisha mchakato wa kupeleka elimu ya rushwa shule za msingi, sekondari vyuoni

 MOSHI-KILIMANJARO

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amezielekeza Wizara za Elimu Sayansi na Teknolojia na ile ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kuendelee kukamilisha mchakato wa usambazaji wa vitabu kwenye shule zote za msingi, sekondari na vyuo ili somo la historia na maadili ya mtanzania lianze kufundishwa ifikapo Januari mwaka 2025.

Waziri Mkuu Majaliwa ametoa maelekezo hayo  mnamo Oktoba 26,2024, wakati  akifunga mafunzo maalumu ya Awali ya Uchunguzi kwa Maofisa Wapya 436 Wachunguzi na Wachunguzi Wasaidizi wa Takukutu yaliyofanyika katika shule ya Polisi Tanzania  mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro

“Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na Ofisi ya Rais Tamisemi, iendelee kukamilisha mchakato wa usambazaji wa vitabu kwenye shule zetu, ili somo la historia na maadili ya Mtanzania lianze kufundishwa ifikapo mwezi Januari 2025.”amesema.

Ameongeza kuwa “Sera mpya inaeleza lengo la Serikali ni kujenga kizazi chenye maadili na uzalendo na chenye kuchukia rushwa.”

Aidha ameitaka Takukuru iendelee kuongoza ufuatiliaji na usimamizi wa karibu wa fedha zinazotolewa na serikali kwa ajili utekelezaji wa miradi mbalimbali, pamoja na fedha zinazotolewa na taasisi binafsi kwenda kwa wananchi kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo. “Wabadhilifu wa fedha za maendeleo waainishwe, wabainike na waendelee kuchukuliwa hatua zinazostahiki, nilipata ziara ya kutembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo kwenye wilaya, niliyakuta haya, lakini nashukuru sana maeneo yote niliyopita nilipata ushirikiano mzuri kutoka kwenye taasisi yetu ya Takukuru, kupitia makamanda wa wilaya na mikoa hongereni sana."

Aidha Waziri Mkuu amewahakikishia Watanzania kuwa Seriakli itaendelea kuwa dhidi ya wala rushwa, itaendelea kuwa wakali dhidi ya idara za ununuzi zinazochepusha fedha za maendeleo.

“Makamand nendeni mkawe wakali dhidi ya Watumishi wa umma wanaopindisha matumizi ya fedha za miradi zinazopelekwa na serikali kwenye maeneo ya wananchi.”amesisistiza.  Kuhusu wahitimu hao, Waziri Mkuu Majaliwa amewataka kwenda kufanya kazi kwa weledi, huku wakizingatia Sheria na kanuni zinazohusiana na shughuli zao huku wakishirikiana na wananchi wenye nia njema na nchi yetu.

Awali akitoa taarifa za taasisi hiyo Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Nchini (Takukuru) Crispin Chalamila amesema jumla ya watumishi wapya wa taasisi hiyo 436 wamehitimu mafunzo hayo ya awali ambayo amesema ni ya lazima kwa maofisa wapya wanaojiunga na taasisi hiyo.

Akimkaribisha Waziri Mkuu, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejiment ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, George Simbachawene, amewataka wahitimu hao kujituma wakati wakitekeleza majukumu yao ili kuakisi juhudi kubwa  zinazofanywa na Serikali katika kuiimarisha Takukuru ikiwemo kwa kuipatia vitendea kazi na kuongeza nguvu kazi kupitia ajira mpya.

Wakati wa halfa hiyo,Waziri Mkuu aliukabidhi uongozi wa Takukuru magari mapya 88 ambayo yatasambazwa nchini kote, hayo yakiwa ni sehemu ya magari zaidi ya 195 ambayo Serikali imeyaagiza ili kuiimarisha taasisi hiyo.








Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.