MOSHI-KILIMANJARO
Elimu ni jambo la muhimu
sana ambalo huchochea maendeleo ya watu binafsi na ya nchi kwa ujumla, pamoja
na umuhimu wake huo sekta ya elimu, imekubwa na changamoto mbalimbali hususani
kwa watoto wa kike
Moja wapo ya changamoto
hiyo ni watoto kutembea umbali mrefu kutoka nyumbani hadi shuleni hasa kwa
wanafunzi wa kike wanaosoma shule za sekondari, ambao wamekuwa wakikumbana na
vishawishi vingi, vinavyopelekea kwao kukatisha masomo yao
Akizungumza Gladness
Kimaro, mwanafunzi wa shule ya sekondari TPC anasema, mara nyingi amekuwa akikatishwa
tamaa ya kusoma kutokana na kutembea umbali wa kilometa 12 na kutawaliwa na
hofu ya kuadhibiwa na mwalimu kwa kuchelewa kufika shuleni baada ya kutembea
muda mrefu.
“Mradi huu wa bweni kwa
wanafunzi wa kike ambalo tumejengewa na Shirika la FTK, limetusaidia sana
kutupunguzia changamoto ya kutembea umbali mrefu.”amesema.
Mwanafunzi mwingine wa kidato cha pili Esther Edgar shule ya
sekondati TPC anasema umbali wa kutoka nyumbani hadi shuleni ni kulometa 10,
ilikuwa inapelekea changamoto ya kuchelewa kufika shulenina hivyo kupoteza
vipindi na ufaulu wake kushuka.
Elisipegwa Kitundu mwanafunzi
wa kidato cha tatu, amesema alikuwa analazimika kutembea umbali wa kilometa 15
kutoka kijiji cha Kikavu hadi shuleni.
Amesema kabla ya kujengwa
kwa bweni hilo, alikuwa hafanyi vizuri kitaaluma kwenye masomo yake kutokana na
kufika akiwa amechoka na hivyo kushindwa kujisomea
Mwanafunzi wa kidato cha
nne Liliani John, amesema alikuwa akitoka nyumbani saa kumi na moja alfajiri na
kufika shuleni saa tatu asubuhi kutokana na changamoto ya usafiri, ambapo usafiri
ambao ulikuwa unapatikana ni malori ya kubeba mchanga, wakati mwingine
wanakataa kukubena na wengine wanapombeba wanamtaka kingono.
Kwa kutambua changamoto
hizo Shirika lisilokuwa la Kiserikali kutoka nchini Uholanzi lililoko mkoani
Kilimanjaro (FTK) limekabidhi miradi miwili ya maendeleo kwa wakazi
wanaozunguka Kiwanda cha Sukari TPC, kilichopo Wilaya ya Moshi Vijijini ikiwa
ni sehemu ya kurudisha kwa jamii.
Akizungumza wakati wa hafla
ya kukabidhi bweni na maktaba kwa shule ya shule ya sekondari TPC Meneja Huduma
za Jamii wa Kiwanda cha Sukari TPC na Msimamizi wa Shirika la FTK Lazaro Urio,
amesema shirika hilo limekabidhi miradi miwili ya maendeleo ikiwemo bweni la
watoto wa kike pamoja na maktaba kwa shule hiyo, ikiwa ni sehemu ya kurudisha
kwa jamii.
Urio amesema FTK kwa kushirikiana
na Kiwanda cha Sukari TPC wamekuwa wakifanya kazi kwa pamoja ili kupunguza
changamoto hizo kwa kutekeleza na kutengeneza mazingira rafiki, salama na
wezeshi kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari ili kuchochea upatikanaji
wa elimu bora na maendeleo ya nchi kwa ujumla
Amesema ujenzi wa bweni
umegharimu kiasi cha Sh milioni 147, ambapo lina uwezo wa kuchukua watoto 64 wa
kike huku ujenzi wa maktaba ukigharimu kiasi cha Sh milioni 126, ambayo ina
uwezo wa kutumiwa na wanafunzi 48.
Kwa upande wake Mwenyekiti
wa Bodi ya FTK, Jaffary Ally, amesema taasisi hiyo inatumia zaidi ya Sh bilioni
1 kila mwaka kwa ajili ya huduma za jamii katika Wilaya za Moshi Vijijini, Hai
mkoani Kilimanjaro, pamoja na Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara.
Kuhusu ujenzi wa bweni hilo
Ally, amesema watoto wengi wa kike walikuwa wakirubuniwa kwa zawadi ndogo
ndogo, au kubakwa na watu wenye nia mbaya jambo ambalo liliwaweka kwenye hatari
ya kuambukizwa magonjwa ya zinaa au kupata mimba na kufukuzwa shule.
Naye Mkuu wa Shule ya
Sekondari ya TPC Salehe Mwijuma Shekibwai, amesema awali wanafunzi hao walikuwa
na changamoto nyingi ikiwemo ya kutembea umbali mrefu na kwamba kujengwa kwa
bweni hilo na maktaba, imeleta manufaa makubwa sana kwa wanafunzi hao.