FTK yawaondolea adha wanafunzi 1,000 waliokuwa wakitembea umbali wa kilometa 20 kusaka elimu

MOSHI-KILIMANJARO

Zaidi ya wanafunzi 1,000 wa kata zilizoko Halmashauri ya Wilaya ya Moshi (MDC) na ambazo ziko jirani na Kampuni ya kutengeneza Sukari ya TPC Limited ya mjini Moshi mkoani Kilimanjaro, wamekwepa adha ya kusafiri umbali mrefu kwenda na kurudi shuleni, baada ya uanzishwaji wa shule mbili za Sekondari katika eneo la TPC Ltd.

Hayo yamesemwa Oktoba 25, 2024 na Msimamizi wa Shirika lisilo kuwa la Kiserikali la FTK  Lazaro Urio, wakati wa hafla ya kukabidhi Mabweni na Maktaba kwa shule ya Sekondari TPC, ambayo ni kitengo cha uwajibikaji kwa Jamii (CSR) cha Kiwanda cha Sukari TPC iliyofadhili ujenzi wa shule, mabweni na miradi ya maktaba.

“Kabla ya ujenzi wa shule hizo, wanafunzi wengi wao wakiwa ni watoto wadogo walilazimika kutembea umbali mrefu kufika shule zilizo nje ya eneo la TPC”, alibainisha na kuongeza, ndipo wazo la kuanzishwa kwa shule mbili za sekondari za TPC na Shule ya Sekondari ya Chewe katika eneo hilo ilianzishwa.

 Urio amesema kuwa, baada ya kujengwa kwa shule hizo mbili, changamoto nyingine iliibuka ambapo amesema, safari hii wanafunzi wengi kutoka nje ya eneo la TPC walilazimika kutembea umbali wa kilomita 14 hadi 20 kwenda na kurudi kutoka katika shule hizo mbili.

"Ili kukabiliana na changamoto hiyo, FTK ilikuja na wazo lingine la kulipia usafiri wa wanafunzi kwa kukodisha mabasi, ambapo wazazi walialikwa kuchangia asilimia 50 ya gharama, lakini wengi hawakuweza kufanya hivyo kwa sababu mbalimbali", amesema.

Kwa mujibu kiongozi huyo, kufuatia changamoto hiyo mpya FTK ilikuja na wazo la ziada la kujenga bweni katika shule ya Sekondari ya TPC litakalohifadhi wanafunzi 64 waliokuwa wakitembea umbali mrefu kwenda na kurudi shule ya sekondari ya TPC.

“FTK iliamua kuwekeza katika shule ya Sekondari ya TPC kwa kujenga bweni jipya lenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 64 kwa  gharama ya shilingi milioni 147, ambapo uongozi wa shule ulipewa jukumu la kuweka vitanda kwa ajili ya bweni hilo”, amesema Urio.

Kuhusu maktaba mpya ya shule hiyo, Urio amesema ujenzi wake umegharimu Sh milioni 126 na kwamba itajumuisha maabara ya kompyuta.

“Maktaba hii haina samani hivyo nitoe rai kwa wadau mbalimbali kuungana na FTK kukusanya jumla ya Sh milioni 25 ili kumudu gharama za samani zote zinazohitajika katika maktaba hiyo mpya”, amesema. 

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mwenyekiti wa Bodi ya FTK, Jaffary Ally, amesema taasisi hiyo inatumia zaidi ya Sh  bilioni 1 kila mwaka kwa ajili ya huduma za jamii katika wilaya za Moshi Vijijini na Hai zilizoko mkoani Kilimanjaro, pamoja na Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara.


Mwenyekiti wa Bodi ya FT-Kilimanjaro Jaffary Ally, akizungumza na Waandishi wa habari hawapo katika picha mara baada ya kukabidhi miradi miwili ya mabweni na maktaba katika shule ya sekondari TPC 
Wadau wa Maendeleo kutoka Uholanzi, wakiwa katika eneo la shule ya Sekondari TPC 
Wanafunzi wa Shule ya Sekondari TPC wakiwa wanajisomea 
Jengo la Maktaba lililogharimu kiasi cha Sh milioni 126, ambalo lina uwezo wa kutumiwa na Wanafunzi 48.
Bweni lenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 64 wa kike limejengwa na Taasisi isiyo kuwa ya kiserikali ya FT-Kilimanjaro na kugharimu kiasi cha Sh milioni 147.


Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.