Mbunge wa Mwanga Joseph Tadayo, ahamasisha utalii wa ndani..

MWANGA-KILIMANJARO

Mbunge wa Jimbo la Mwanga mkoani Kilimanjaro Joseph Tadayo ametoa wito kwa Watanzania kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii ili kukuza utalaii wa ndani, badala ya kutegemea watalii kutoka nje ya nchi.

Ametoa wito huo Oktoba 27/2024, wakati akizungumza na Waandishi wa habari mjini Moshi, kuhusu namna ya kukuza sekta ya utalii nchini hususani utalii wa ndani.

“Sekta ya utalii hapa nchini ikiwemo wilaya ya Mwanga inaendelea kukua siku hadi siku kwa kupitia maono ya rais Samia Suluhu Hassan hasa kwa kupitia filamu yake ya Royal Tour,” amefafanua Tadayo.

Mbunge huyo ameendelea kusema kuwa, Wilaya ya Mwanga kwa kushirikiana na Wadau Utalii, imeandaa Tamasha Maalumu la kukuza Utalii ikiwemo Mbio Maalumu ya Mwanga Festival and Marathon 2024 ambayo itayofanyika mwezi  Desemba 27 mwaka huu.

“Mbio hizo zitakuwa za kilometa tano, zitaanzia uwanja wa Cleopa Msuya na kutamatika katika Gereza la Kilulu na nitumie nafasi hii kuwashukuru wadau mbalimbali wakishirikina na halamashauri ya wilaya ya Mwanga kufanikisha Tamasha hili ikiwemo familia ya Mberesero kupitia   kupitia taasisi ya Kisangara Tours,” amesema Tadayo.

Ameendelea kufafanua kuwa, Mbio hizo zitakuwa na faida nyingi sana katika kukuza sekta ya utalii, hususani utalii wa ndani katika wilaya ya Mwanga na hivyo kukuza uchumi.

Amesema wilaya ya Mwanga ina vivutio vingi vya utalii ambavyo havitangazwa sana na kuongeza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imejenga mazingira rafiki ya uwekezaji ambapo sekta binafsi zimevutiwa sana kuwekeza kutokana na utendaji wake  mzuri.

“Katika wilaya yetu ya Mwanga kuna vivutio mbalimbali vya utalii ambavyo havijatangazwa sana ikiwemo Jiwe linaloitwa ‘Mkumbavana’ ambapo watoto walipokuwa wakizaliwa na changamoto ikiwemo ya ulemavu walikuwa wakipelekwa na kutupwa na kufia huko ambapo Wajerumani walipokuja walianza kuwaelimisha watu na kuacha tabia hiyo.” amefafanua mbunge huyo.

Pia Tadayo aliendelea kufafanua kuwa, Mtunzi asilia wa wimbo wa maarufu wa Kizalendo wa ‘Tanzania, Tanzania, Nakupenda kwa moyo wote, ulitungwa na Mchungaji Sila Msangi mzaliwa wa Kata ya Kifula Wilayani humo.

Kwa upande wake, Mkuu wa wilaya ya Mwanga Mwanahamisi Munkunda ametoa wito kwa wananchi wa wilaya ya Mwanga kujitokeza kwa wingi kwenye tamasha hilo maalumu.

“Pia ninatoa wito kwa wana-Mwanga wanaoishi Ughaibuni (Diaspora) pindi watakapokuja kujumuika na familia zao katika sikuu za mwisho wa mwaka kushiriki katika tamasha hilo,” amesisitiza mkuu huyo wa wilaya.





Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.