Watu Ml 1 kushiriki Uchaguzi Serikali za Mitaa Kilimanjaro

MOSHI-KILIMANJARO.

Jumla ya watu 1,090,312 wamejiandikisha mkoani Kilimanjaro kwa ajili ya kushiriki uchaguzi wa Serilali za Mitaa mkoani unaotarajiwa kufanyika Novemba 27, mwaka huu.

Hayo yameelezwa Oktoba 21,2024 na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Nurdin Babu, wakati akitoa taarifa inayohusiana na zoezi hilo, ambapo amesema idadi hiyo ni asilimia ya lengo lililowekwa la kuandikisha watu 1,172,394.

“Kati ya waliojiandikisha ni wanaume walikuwa 544,189 na wanawake ni 546,123 na kwamba wilaya ya Mwanga ndiyo iliyoongoza kimkoa, kwa kuvuka malengo yaliyowekwa ya uandikishwaji wilayani humo”, amesema.

Ameongoze, “Halmashauri ya wilaya Mwanga iliandikisha jumla ya watu 92,112 sawa na asilimia 100.9 ya lengo lililokuwa limewekwa la kuandikisha watu 91,327”.

Kwa mujibu wa Babu, halmashauri za wilaya zingine ni pamoja na Same iliyoandikisha watu 180,649 sawa na asilimia 100.0 ya lengo la kuandikisha watu 180,587.

Babu amezielezea takwimu za uandikishwaji za halmashauri za wilaya zingine na malengo yake kwenye mabano kuwa ni Siha 79,749 (81,501), Moshi Manispaa 144,213 (149,937) na Rombo 155,601 (171,330).

Aidha amezitaja halmashauri zingine kuwa ni Halmashauri ya wilaya ya Moshi (Moshi-DC) 306,178 (344,715) na kwamba halmashauri ya wilaya ya Hai imeandikisha jumla ya watu 131,810 ikilinganishwa na malengo ya kuandikisha watu 152,997.

Katika hatua nyingine Babu ametoa shukrani kwa watu waliojitokeza katika kushiriki zoezi la uandikishwaji kwa ajili ya kujiandaa kwa uchaguzi utakaofanyika baadaye mwaka huu.

“Nitoe wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi huo wakati wa kuchukua fomu na hata kampeni zitakapoanza.”amesema Babu.

Amesema “Uchaguzi huu una faida kubwa kwa wananchi kutokana na ukweli kuwa viongozi watakaochaguliwa ndiyo wenye dhamana ya kushughulikia shughuli za kimaendeleo kwenye maeneo wanayotoka”, amesema.

Ameongeza, “Viongozi wa ngazi za mitaa ndiyo waliokaribu zaidi na wananchi, hivyo wao ndiyo wa kwanza kujua mahitaji ya wananchi ya kimaendeleo; wakishabaini mahitaji husika ndiyo serikali kuu nayo inakuja na mipango ya kuleta maendeleo hayo”.

Wakizungumzia mchakato huo wa uandikishaji wa wapiga kura kwenye daftari la wapiga kura Mwenyekiti wa Chama cha Sauti ya Umma (SAU) mkoani Kilimanjaro Isaack Kireti na Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) Wilaya ya Moshi Habibu Hamisi Msangi, wamesema kuwa zoezi hilo limekwenda vizuri.

“Kikubwa tulichokibaini hapa ni uhamasishaji mkubwa uliofanywa na mamlaka husika kwa wananchi wajitokeza kujiandikisha; haijawahi kutokea uhamasishaji wa aina hii kwa miaka mingi iliyopita”, wamesema.

Aidha viongozi hao wametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi zilizoko ili wapatikane viongozi ambao wako karibu na wananchi na ambao watakuwa tayari wa mbele kuwahudumia wananchi.

 

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.