Halmashauri ya Mwanga yavunja rekodi ya uandikishaji wa orodha ya wapiga kura Serikali za Mitaa

MOSHI-KILIMANJARO.

Halmashauri ya Wilaya ya Mwanga mkoa wa Kilimanjaro, imevunja rekodi ya uandikishaji wa orodha ya Wapiga Kura, Uchaguzi wa Serikali za Mitaa  na hivyo kusika nafasi ya kwanza kimkoa.

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Nurdin Babu, ameyasema hayo Oktoba 21,2024 wakati akitoa taarifa inayohusiana na zoezi hilo kwa waandishi wa habari ofisini kwake, ambapo amesema halmashauri ya Wilaya Mwanga iliandikisha jumla ya watu 92,112 sawa na asilimia 100.9 ya lengo lililokuwa limewekwa la kuandikisha watu 91,327.

Kwa mujibu wa Babu, amesema halmashauri iliyoshika nafasi ya pili ni Same iliyoandikisha watu 180,649 sawa na asilimia 100.0 ya lengo la kuandikisha watu 180,587.

Amesema nafasi ya tatu imeshikwa na halmashauri ya Wilaya ya Siha iliyoandikisha watu 79,749 sawa na asilimia 97.9 huku nafasi ya nne ikishikwa na Halmashauri ya Manispaa ya Moshi ambayo iliandikisha watu 144,213 sawa na asilimia 96.2 ambapo makadirio ilikuwa ni kuandikisha watu (149,937).

Babu alizielezea takwimu uandikishwaji za halmashauri za Wilaya zingine na malengo yake kwenye mabano kuwa ni Rombo watu 155,601 sawa na asilimia 90.8, ambapo malengo ilikuwa ni kuandikisha watu  171,330.

Aidha amezitaja halmashauri zingine kuwa ni Halmashauri ya Wilaya ya Moshi (Moshi-DC) watu 306,178 sawa na asilimia 88.8 (344,715) na kwamba halmashauri ya Wilaya ya Hai imeandikisha jumla ya watu 131,810 sawa na asilimia 86.2, ikilinganishwa na malengo ya kuandikisha watu 152,997.

 

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.