Mkuu wa wilaya ya Moshi, awaonya vijana usafirishaji wa dawa za kulevya

MOSHI-KILIMANJARO

Mkuu wa Wilaya ya Moshi James Kaji, amewataka Vijana kuachana na matumizi ya dawa za kulevya na badala yake waungane katika kufanya shughuli halali za kiuchumi ili wajiletee maendeleo katika ngazi ya familia, jamii na hata Taifa.

Kauli hiyo jana, wakati akizungumza kwenye Tamasha la ‘Vijana na Uongozi Festival’ lililofanyika kwenye viwanja vya Polisi Himo na kuhudhuriwa na vijana takribani 200 kutoka kata 32 za Wilaya hiyo.

Kaji amesema kwa sasa kuna wimbi kwa  baadhi ya vijana kutumika kusafirisha bange, mirungi na kuwaonya kujiepusha kabisa na usafirishaji wa dawa za kulevya kwani wakikamatwa wataishia gerezani.

“Kwa Wilaya yetu ya Moshi  tatizo hili  la vijana kutumika kusafirisha mirungi, bangi na wahamiaji haramu ni kubwa, watu wasilifumbie macho, kwa taarifa za polisi kila  kila siku, wanaokamatwa na usafirishaji wa dawa za kulevya aina ya mirungi na bangi  vi vijana,”amesema.

Amesema wako pia baadhi ya vijana wanatumika kusafirisha wahamiaji haramu kuwavusha mpakani na kuwahifadhi, ulevi wa gongo kupindukia, tatizo hili ni kubwa sana katika wilaya ya Moshi.

Aidha mkuu huyo wa wilaya  ametoa rai vijana ambao hamjaingia kwenye usafirishaji wa dawa hizo, lakini pia na utumiaji wa pombe aina ya gongo, wasishawishike  kuingia huko na  wale ambao wameshaathirika na dawa amewataka kuendelea kutumia dawa za kuwakinga ili wasiathirike zaidi.

Katika hatua nyingine Kaji, alitumia fursa ya tamasha hilo kuwataka vijana kuwa na maadili mema pomoja na kujiepusha na makundi ya ushawishi ili kulinda afya zao na nguvu kazi ya taifa.

“Nitumia tamasha hili kuwataka vijana mjikite zaidi na Shughuli za kimaendeleo, ikiwemo ufugaji, kilimo na ujasiriamali, lakini pia nendeni mabalozi wazuri  kwa kuwaelimisha wale wote ambao hawakupata nafasi ya kushiriki katika tamasha hili, kuhusu athari na madhara ya matumizi ya dawa za kulevya kwa ustawi wa jamii na Taifa kwa ujumla.”amesema.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa UVCCM Wilaya ya Moshi vijijini Yuvenari Shirima, alisema kupitia tamasha hilo pia vijana watapatiwa elimu ya fedha ili kuwajengea uwezo wa kufanya maamuzi sahihi ya kupata na kutumia huduma za fedha hapa nchini.

“Elimu ya Fedha ni program inayotolewa kwa kuzingatia mwongozo wa mkakati wa maendeleo ya Sekta ya Fedha, ziko taasisi mbali za kifedha zitakwenda kuwapatia elimu juu ya masuala elimu ya fedha na mwongozo huo ambao pamoja na mambo mengine ni lazima vijana hawa wapate elimu ya fedha katika makundi mbalimbali kama vile Vyama vya Ushirika, Wanafunzi, Waalimu, Wafanyakazi, Vikundi vya huduma ndogo za fedha na Wananchi kwa ujumla.”amesema.

Ameongeza kuwa Rais Samia ameruhusu kuanza kutolewa kwa mikopo isiyokuwa na riba kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu na kwa halmashauri ya halmashauri ya Moshi kuna zaidi ya milioni 800.

Naye Katibu wa UVCCM Wilayani humo Malkiori Pantaleo, amekiri kuweko kwa baadhi ya vijana kujiingiza kwenye unywaji wa pombe aina ya gongo kupindukia.




 

 

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.