Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWT) lapongezwa kwa kuonesha ukakamavu, uzalendo na umahiri

Kikosi maalumu cha Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWT) kilichokuwa kimepandisha Mwenge wa Uhuru na Bendera ya Taifa katika kilele cha mlima Kilimanjaro.

MOSHI-KILIMANJARO

Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Dkt. Stergomena Tax, amekipongeza kikosi maalumu cha Jeshi la Wananchi Tanzania (JWT) kwa kuonesha ukakamavu, uzalendo na umahiri katika kufikisha Mwenge wa Uhuru pamoja na Bendera Taifa kwenye kilele cha mlima Kilimanjaro.

Waziri Tax ametoa pongezi hizo Oktoba 21, 2024, wakati wa kukipokea kikosi hicho kilichopandisha Mwenge wa Uhuru na Bendera ya Taifa katika kilele cha mlima Kilimanjaro, hafla iliyofanyika katika Geti la Marangu Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjro na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro pamoja na Watendaji wa Taasisi za Serikali.

Waziri Dkt. Stergomena Tax amesema kuwa, kupandishwa kwa Mwenge wa Uhuru kwenye kilele cha mlima Kilimanjaro ni ishara ya kusherehekea miaka 60 ya historia yetu na kutukumbusha wajibu wa kulinda Uhuru kwa kujenga Taifa lenye Umoja, Mshikamano, na Maendeleo.

“Naomba niwapongeze sana kwa kazi nzuri wanayoifanya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWT) kazi mnayoifanya ni kubwa, ambapo sote tuna Amani, Taifa letu liko Imara, tunao mshikamano, mipaka yetu iko salama si kwa sababu iko salama tu…ni kwasababu ya kazi kubwa inayofanywa na Jeshi letu hili,”amesema.

Akizungumza katika hafla hiyo Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Jacob Mkunda, amesema, ametekeleza agizo alilopewa kwa uangalifu mkubwa na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan.

“Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama Dkt. Samia Suluhu Hassan, alinipatia Jeshi la Wananchi wa Tanzanaia, jukumu la kupeleka Bendera ya Taifa na Mwenge wa Uhuru kupeleka katika kilele cha mlima Kilimanjaro,   mimi kama CDF nilipokea jukumu hili kwa niaba ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania,”amesema,

Ameongeza kuwa “Jeshi la Wananchi wa Tanzania limetekeleza agizo la Amiri Jeshi Mkuu kwa weledi, uaminifu na uangaligifu mkubwa.”amesema.

Aidha Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Jacob Mkunda, ametoa shukrani kwa Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro kwa kutoa ushirikiano muhimu kwa timu nzima.

Oktoba 14, 2024, Rais Samia Suluhu Hassan alimkabidhi Mwenge na Bendera ya Taifa Jenerali Mkunda ili Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWT) waweze kupandisha Mwenge wa uhuru na Bendera ya Taifa katika kilele cha mlima Kilimanjaro, ambapo  safari  ya kuupandishi Mwenge wa Uhuru ilianza Oktoba 15 na kukamilika rasmi Oktoba 21, kwa furaha kubwa baada ya mafanikio ya kurejesha Mwenge salama.









Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.