Wananchi waliobomolewa nyumba zao, kupisha ujenzi wa barabara ya Same-Kisiwani-Mkomazi kwa kiwango cha lami, walalamikia kutolipwa fidia walizoahidiwa awali

Miongoni mwa nyumba iliyobomolewa kupisha mradi wa ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami.

SAME-KILIMANJARO

WANANCHI wa tarafa za Gonja, Ndungu na Bendera, Wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro, wamemuomba Rais Samia Suluhu Hassan, kuingilia kati swala la wao kutokulipwa fidia baada ya kutakiwa kuvunja nyumba zao ili kupisha ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami.

Wakiongea na Waandishi wa habari kuhusiana na swala hilo, wananchi hao wamesema kuwa swala hilo limewasababishia usumbufu mkubwa na kwamba Rais tu ndiye anayeweza kuwasikiliza ili wapate haki zao.

Mkazi wa Kata Ndungu Mlavi Mohamed, amesema kuwa waliarifiwa kuwa kuna mradi huo wa barabara ambao utaenda sambamba na upanuzi wa barabara hiyo ya Same-Kisiwani-Mkomazi.

“Mara ya kwanza walikuja wakapima, wakaja wakatufanyia tathmini wakatupiga picha, wakatuambia watatulipa, baada ya hapo wakaja tena kwa mara ya pili wakatuambia hatutalipwa na wakatupa muda wa siku 30 wakitutaka tuvunje nyumba zetu,”amesema Mohamed.

Ameongeza kuwa “Hali hii imeniathiri sana kiuchumi, nimebomoa nyumba zangu saba ambazo zote zilikuwa na wapangaji,  ambao walikuwa wamelipa kodi zao,”amesema.

Akisimulia zaidi Mohamed, amesema kuwa mara ya kwanza walikuja wapimaji wakapima nyumba zilizokuwa eneo la barabara zikawekewa alama za kuonyesha kuwa ziondolewe ambapo waliambiwa watalipwa fidia.

“Mara ya pili wakaja wapimaji wengine ambao walipima na kuongeza idadi ya nyumba ambazo hazikuwekewa lama ya kuondolewa mara ya kwanza na hizi tumeambiwa wahusika wake hawatalipwa fidia”, amesema.

“Tumepewa mwezi mmoja kuziondoa nyumba zetu wenyewe na baada ya hap wale ambao hawakuwa wameziondoa nyumba zao zitaondolewa na kisha wenye nyumba hizo tumeambiwa tutatakiwa kuwalipa fidia wale watakaokuja kuzivunja”, amesema.

Mkazi huyo alihoji ni kwanini upimaji umefanyika mara mbili na ile ya pili hawatalipwa fidia na tena waziondoe wenyewe huku wakitishiwa kuwa zitavunjwa na mamlaka husika halafu tuwalipe kazi hiyo kuvunja nyumba zetu.

“Tunachojiuliza hapa ni je, wale waliopima kwanza si wa serikali? Na kama ni wa serikali ni je hawajui kazi zao kiasi cha kwamba wananchi tunapata usumbufu usio na sababu?”, alihoji mkazi huyo.

Mkazi wa Ndungu Sufiani Mvule, amesema suala la ujenzi wa barabara katika Jimbo la Same Mashariki, limekuwa ni suala la wana siasa kujitafutia mtaji wao wa kupata kura.

“Bomoa bomoa inayoendelea imetuathiri kwa kiasi kikubwa sana, kwanza namna notisi iliyotolewa ni ya muda wa mwezi mmoja, wako baadhi ya watu kwa sasa wamehifadhiwa na ndugu zao kwa kuwa hawana tena hela za kujenga.”amesema.

Wakazi wengine wa kata ya Bendera Zakia Richard na Rabia Haji, wamesema kuwa wanapenda kuwa na maendeleo, ila kilio chao kifikiriwe maana wao kama Watanzania wengine wana haki ya kuwa na makazi mazuri hata kama watatoa maeneo yao kwa ajili ya maendeleo.

“Ni kweli mradi huu wa barabara ni swala la kimaendeleo na hata shughuli za kibiashara zitakuwa, ila tunachoomba mamlaka husika iweze kutulipa fidia ili tuweze kujenga nyumba nyingine za kuishi”, wamesema.

Mwananchi mwingine Asha Bakari Kibwana mkazi wa Ndungu, amekiri kupokea notisi ya mwezi mmoja inayomtaka avunje nyumba yake ndani ya siku 30 ili kupisha ujenzi wa barabara hiyo.

Amesema alifiwa na mwanae  mwezi Julai 27 na kumzika Julai 29 mwaka huu na ilipofika mwezi Agosti 6 mwaka huu aliletewa notisi ya kutakiwa kubomoa nyumba yake ili kupisha ujenzi wa barabara.

“Mimi maendeleo sikatai, ila tunachokiomba serikali iweze kutupa fidia ili tuweze kwenda kununua maeneo mengine tuweze kujenga, lakini cha kushangaza wametuletea notisi ya kututaka tubomoe nyumba na fidia wamesema hatutalipwa,”alisema.

Alipotakiwa kuzungumzia swala hilo Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) mkoani Kilimanjaro Mhandisi Motta Kyando amesema hayuko tayari kuzungumzia swala hilo kwa sasa kutokana na kuwa swala hilo liko ngazi ya juu kiofisi.

Aidha Kyando, amesema ujenzi wa barabara hiyo ukikamilika utafungua uchumi wa wakazi wa Wilaya ya Same, ambao kwa kiasi kikubwa wanategemea shughuli za kilimo cha mazao ya tangawizi, mpunga na ndizi  na kuhuisha utalii katika Hifadhi ya Taifa ya Mkoamazi.

“Barabara ya Same-Kisiwani –Mkomazi ina urefu wa kilometa 98 inatarajiwa kugharimu kiasi cha Sh bilioni 68 na kwamba kukamilika kwake itatoa fursa za kiuchumi na utalii kwa wananchi wa ukanda wa milimani ambao wengi ni wakulima wa mazao mbalimbali ikiwemo Tanzngawzi, mpunga na mazao mengine.

Kuhusu barabara ya Ndungu-Mkomazi, Mhandisi Kyando alisena ina kipande cha kilometa 36.9, ambapo tayari serikali kupitia Wakala wa Barabara imesaini mkataba wa kuweza kuanza kazi ya ujenzi kwa kiwango cha lami.

“Mkataba huu ulisainiwa mwezi Januari mwaka huu, ambapo mradi huo utachukua miezi 18 na kwamba ifikapo mwezi Desemba mwaka 2025 kazi ya ujenzi itakuwa imekamilika.”amesema.

Mhandisi Kyando ameongeza kusema kwamba barabara hiyo endapo itakamilika itakuwa na manufaa makubwa sana, kwani kutakuwa na maendeleo makubwa  kwa, vijana  ambao watapata ajira na kukuza  uchumi baada ya watalii kuongezeka na watu wataona urahisi wa kufika katika hifadhi ya mkomazi.

Mkazi wa Ndungu Bi. Asha Bakari Kibwana, akionesha eneo ilipokuwa nyumba yake iliyobomolewa kupisha ujenzi wa barabara

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.