Shirima: Awataka vijana kugombea nafasi za uongozi


Mwenyekiti wa (UVCCM ) Wilaya ya Moshi Vijijini Yuvenari Shirima, akizungumza kwenye Tamasha la Vijana na uongozi , lililofanyika katika viwanja vya polisi himo katika Kata ya Makuyuni kwa lengo la kuwahamasisha vijana kujitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi Serikali za Mitaa 2024

MOSHI-KILIMANJARO

Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) Wilaya ya Moshi Vijijini, umewataka Vijana Wilayani humo, kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi mbalimbali za uongozi katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika Novemba 27 mwaka huu.

Mwenyekiti wa (UVCCM) Moshi Vijijini Yuvenari Shirima, ametoa
 wito huo Oktoba 19, 2024 wakati akizungumza kwenye Tamasha la ‘Vijana na Uongozi Festival’ lililofanyika kwenye viwanja vya Polisi mji mdogo wa Himo na kuhudhuriwa na vijana takribani 200 kutoka kata 32 za Wilaya hiyo.

Shirima amewashauri vijana kuacha kulalamika kwamba hawapewi nafasi za uongozi na kuwataka  wajitokeze kuchukua fomu za kugombea nafasi mbalimbali ili wapate nafasi za kuongoza nchi yao kwa vyeo mbalimbali ikiwemo ya Uenyekiti wa Serikali za Vijiji, Vitongoji na Mitaa kwani nao wana mawazo chanya.

Aidha amesema Chama cha Mapinduzi (CCM) kinawapa fursa vijana wote kugombea nafasi mbalimbali za uongozi kwani Tanzania ya leo na kesho inaundwa na kundi la vijana.

“Serikali iliyopo madarakani chini ya usimamizi wa Rais Samia Suluhu Hassan, imekuwa ikiwatengeneza vijana kuanzia kwenye elimu, kwani inawapa mikopo ya elimu ya juu wasome, lakini pia imetenga fedha kila halmashauri kwa ajili ya mikopo isiyo na riba ili wajikwamua kiuchumi,” amesema Shirima.

Awali akizungumza Katibu wa UVCCM Wilaya ya Moshi Vijijini Malkiori Pantaleo, amesema tamasha hilo ni mwendelezo wa matamasha ambayo wamekuwa wakiyafanya ili  kuwahamasisha vijana kujitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

“Lengo la tamasha hili ni kuwahamasisha vijana kujitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi na huu ni mwendelezo wa matamasha ambayo tumeshayafanya katika kata za Mwika Kusini, Kibosho na Mwika Kaskazini,”amesema Pantaleo.

Naye Katibu wa UWT Moshi Vijijini Olva Ngalawa, amewahamasisha Wanawake Wilayani humo, kuunga mkono juhudi za Rais Samia Suluhu Hassan za matumizi ya Nishafi safi ya kupikia katika maeneo mbalimbali ili kusaidia kutunza mazingira, kuokoa muda, kuimarisha afya na Uchumi.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Moshi James Kaji, amesema ili waweze kumchagua kiongozi bora atakayewaletea maendeleo katika vijiji na vitongoji vyao vijana hawana budi, kujitokeza kushiriki kugombea nafasi hizo za uongozi.

Tamasha hilo, lilikuwa limebeba Kauli Mbiu ‘Wakati Wetu Ndo Sasa Vijana Tujitokeze Kugombea” ni mwendelezo wa matamasha ambayo UVCCM imekuwa ikiyafanya kwa lengo la kuwahamasisha vijana kushiri Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu mwaka 2024.



















Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.