Ruwasa yaanza kutatua changamoto ya maji Siha.

SIHA-KILIMANJARO

Wilaya ya Siha, imepokea mtambo wa kuchimba visima virefu vya maji, ambapo mtambo huo utakwenda kuchimba visima vya maji katika maeneo kadhaa ya Wilaya hiyo ambayo hayana vyanzo vya maji ya mserereko (mtiririko).

Meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Wilaya ya Siha Injinia Emmy George, amesema hayo Oktoba 14, 2024 ofisini kwake, wakati akizungumza na Waandishi wa habari wilayani humo.

Amesema mtambo huo utakwenda kuchimba visima vitano vya maji vitakavyosaidia kuboresha huduma ya maji katika wilaya hiyo na kuondoa changamoto ya maji katika  baadhi ya vijiji vilivyoko katika wilaya hiyo.

“Ruwasa tuna mpango wa kuanza kuchimba visima vitano katika wilaya yetu ya siha, ambapo tayari tumeshaainisha maeneo ambapo visima hivyo vitachimbwa, kisima cha kwanza kitachimbwa hospitali yetu ya wilaya, kisima cha pili kitachimbwa kati ya kijiji cha Miti miteru au Karimaji, kisima cha tatu Kandashi,”amesema.

Injinia Emmy ameongeza kuwa visima hivyo vitakapo kamilika vitakwenda kuongeza upatikanaji wa maji kwenye mfumo wa maji uliopo kwa sasa.

Aidha amesema kuwa tayari wataalamu kutoka Bodi ya maji Bonde la Pangani (PBWB)  walikwishapita katika maeneo hayo kupima na kubainisha maeneo yanayoweza kuchimbwa na kupatikana maji hayo  na kwamba utekelezaji wa kazi hiyo unakwenda kuanza mara moja ikiwa ni jitihada za kumtua mama ndoo kichwani.

“Mitambo hii inakwenda kuanza kazi katika maeneo ambayo hayana vyanzo vya maji vya mserereko.”amesema Injinia Emmy.

Pia meneja huyo wa Ruwasa wilaya ya Siha, amesema kuwa kwa mwaka 2024 Ruwasa imefanikiwa kukamilisha mradi mmoja wa maji unaohudumia kata ya Ngarenairobi.

“Tumeshakamilisha mradi mmoja wa maji ambao unahudumia Bodi ya Maji ya Lawate- Fuka, ambao tumeutoa kwenye chanzo kipya cha maji mto Sakana, takribani umbali wa kilometa 13 yalipo matenki ya maji.”

Amesema kupitia mradi huo, wananchi wa maeneo ya Sinai ambao walikuwa na changamoto kubwa ya maji kwa sasa wanapata huduma ya maji safi na salama.

Serikali kupitia Wizara ya Maji imeweka mkazo katika kuhakikisha kwamba wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama kwa karibu na maeneo yao.





Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.