MOSHI-KILIMANJARO
Bodi
ya Maji ya Bonde la Pangani (PBWB) umeweka mikakati inayolenga kuzuia uvamizi
wa Mto Rau ili pamoja na mambo mengine kuzuia mafuriko ambayo huathiri watu
wakati wa mvua.
Mkurugenzi
wa Bodi ya Maji ya Bonde la Pangani (PBWB) Mhandisi Segule Segule,
alipotembelea na kukagua usafishaji wa mto Rau unaoendelea, baada ya mafuriko
yaliyotokea mwanzoni mwa mwaka huu kuathiri familia nyingi katika kata za Mji
Mpya na Msaranga Manispaa ya Moshi, mkoani Kilimanjaro.
Amesema
kuwa PBWB pia imepanga mikakati itakayopelekea kulinda mto huo dhidi ya
uchafuzi wa mazingira kwa sababu kuna watu wamegeuza mto huo kuwa sehemu ya
kutupa takataka.
"Huu ni mto ambao maji yake
yanatumiwa na binadamu hivyo uchafuzi wake unaweza kuleta madhara ya kiafya
hivyo ni vyema tukazuia athari zisitokee”, amesema.
Akizungumza
katika ziara hiyo Diwani wa Kata ya Mji Mpya Abuu Shayo, ameishukuru Serikali
kupitia uongozi wa Bodi ya Maji Bonde la Pangani (PBWB) kwa kuchukua hatua
ambazo amesema zitaepusha mafuriko wakati wa mvua siku zijazo.
“Mafuriko
yaliyotokea Aprili 24 mwaka huu, yaliathiri jumla ya kaya 690 katika Kata mbili
za Mji Mpya na Msaranga, wengi wao walipoteza kila kitu baada ya mali zao
kuchukuliwa na maji na mtu mmoja kufariki dunia, ni matumaini yangu baada baada
ya kazi hii madhara kama haya hayatatokea tena," amesema Diwani Abuu.
Aidha
ametoa wito kwa uongozi wa (PBWB) kuweka alama za mipaka (beacon)
zitakazoonyesha mipaka inayotenganisha makazi ya watu na eneo lililotengwa ili
kuepusha uvamizi.
"Kuna
watu wanaodai kuwa maeneo ya karibu na mto Rau ni mali yao wakati dalili zote
zinaonyesha eneo hilo limehifadhiwa; uamuzi wa kuweka alama hizo za mipaka
utaondoa utata", amesema.
Kwa
upande wake, Diwani wa Kata ya Msaranga, Dkt. Charles Lyimo, amesema kuwa ukosefu
wa mipaka kati maeneo ya mto na makazi umesababisha watu kuingia katika maeneo
yasiyokubalika na kufanya shughuli za kibinadamu zinazoathiri mazingira ya mto
Rau.
“Watu
hawa wanafanya shughuli za kilimo zinazoathiri mazingira ya mto Rau ambapo misimu
ya mvua inapofika, mto hufurika na maji kuingia kwenye makazi ya watu na
kusababisha madhara mengi”, amesema.