Mbio za Mwanga Festival Marathon kufanyika Desemba 27,2024


Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Mbio za Mwanga Festival Marathon Frida Mberesero, akizungumzia mbio hizo zitakazo fanyika Desemba 27, 2024 wilayani humo, ambazo zitakwenda sambamba na Tamasha la Utalii Wilayani humo (Mwanga Tourism Festival).

MWANGA-KILIMANJARO

WAKATI wa serikali ikiwa imedhamiria kuhakikisha idadi ya watalii wanaoingia hapa nchini inaongezeka na kufikia milioni tano fikapo mwaka 2025 kutoka milioni 1.8  ya sasa, kumekuwa na mikakati mbalimbali inayofanywa na Serikali pamoja na Wadau wengine katika Sekta ya Utalii hapa nchini.

Mikakati hiyo ikiwemo ule uliotekelezwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa vitendo kwa kushiriki kutengeneza filamu ya Royal Tour, nchini Tanzania imeanza kuzaa matunda kutokana na idadi ya Watalii kuanza kuongezeka.

Mikakati hiyo imekua chachu kwa wadau wengine nao kujitokeza na kuanza kufanya kampeni ambazo zitachangia ongezeko hilo ili kuendelea kuongeza mapato ya Serikali kuptia Sekta ya Utalii hapa nchini.

Moja wapo ya mikakati hiyo ni ule ambao unaandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mwanga, mkoani Kilimanjaro kwa ushirikiano na Kampuni ya Waongoza Watalii ya Kisangara Tours.

Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Matukio hayo Frida Mberesero, anasema kuwa mkakati huo utahusisha uanzishwaji wa Mbio za nyika Wilayani humo zitakazojulikana kama Mwanga Festival Marathon, ambazo zitakwenda sanjari na  Tamasha la Utalii Wilayani humo (Mwanga Tourism Festival) matukio ambayo anasema yatakuwa yanafanyika kila mwaka.

“Madhumuni ya kuanzisha matukio haya mawili ni kuitangaza Wilaya ya Mwanga na vivutio vyake vya utalii, lengo kuu likiwa ni kupeleka ujumbe ya kuwa viko na hivyo kuvutia watalii wengi zaidi kutoka ndani na nje ya nchi”, anasema.

Frida ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kisangara Tours, anaendelea kusema kuwa mkakati huo mbali na uongozi wa Serikali pamoja na Wadau wengine wa Utalii walioko Wilayani humo, pia utawahusisha wananchi wengine wa wilaya ya Mwanga walioko ndani na nje ya nchi (diaspora) ili kuhakikisha linafanikiwa na hivyo kutimiza azma ya kuitangaza Wilaya ya Mwanga.

“Tamasha hili litakuwa linafanyika Desemba ya kila mwaka, kutokana na kuwa katika kipindi hicho cha mwaka watu wengi huwa wako kwenye mapumziko hivyo litawavutia watu wengi kutoka ndani na nje ya Wilaya ya Mwanga”, anasema Mkurugenzi huyo.

Anaendelea kusema kwamba Mwanga Marathon itakuwa ikifanyika tarehe itakayokuwa imepangwa Desemba 27, mwaka huu, na kufuatiwa na Tamasha la Mwanga Tourism Festival, ambalo litafanyika kwa siku mbili mfululizo baada ya Marathon kufanyika.

“Kwa kuanzia, Mwanga Marathon inatarajiwa kufanyika Desemba 27, mwaka huu na kufuatiwa na Festival itakayofanyika kwa siku mbili, Desemba 28 na 29, mwaka huu”, anasema.

“Mbio za Mwanga Marathon zitafanyia katika uwanja wa Cleopa Msuya, ambapo washiriki watakimbia kwa kilomita 5, kutoka uwanja wa Cleopa Msuya hadi eneo la gereza la Kilulu, ambapo pia washiriki wanaweza kufanya hivyo kwa kutembea”, anasema na kuongeza, mipango ya baadaye ni kuwa na mbio za kilomita 21.

Anaongeza, “Baada ya hapo, Mwanga Tourism Festival itafuata siku ya Desema 28 na 29 ambapo linatarajiwa kufanyika eneo la Bwawa ya Nyumba ya Mungu lililoko Mwanga”.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Mwanga Mwanahamisi Athuman Munkunda anasema kuwa uongozi wa Serikali Wilayani humo umejipanga ili kuhakikisha vivutio vya utalii vilivyoko wilayani humo  vinatangazwa ili kukuza Uchumi wa wilaya hiyo kupitia Sekta ya Utalii.

“Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametuonyesha njia kupitia filamu yake ya Royal Tour Tanzania; filamu hiyo ni dibaji; baada ya kutengeneza filamu hiyo na uzinduzi wake, alitoa maelekezo kwa viongozi wote kuhakikisha wanakuja na mikakati inayolenga kutangaza vivuyio vya utalii vilivyoko maeneo yao; mkakati wetu huu unalenga kutekeleza agizo hilo”, anasema DC Munkunda.

Anasema “Wilaya ya Mwanga inavivutio vingi vya utalii, ikiwemo Bwawa la Nyumba ya Mungu, Ziwa Jipe, Ngoma za Kipare na Utamaduni wa kabila la Kipare kwa ujumla ambavyo vikitangazwa ipasavyo na kupitia mbio hizo Wialaya yetu itakuwa ikipokea wageni wengi kutoka ndani na nje ya nchi kila mwaka na hivyo kukuza Uchumi wa wilaya ya Mwanga.”anasema.

Naye Katibu wa Kamati ya Maandalizi ya matukio hayo Zawadi Mirambo, anasema kuwa maandalizi ya mbio hizo na Tamasha hilo yamefikia asilimia 60, na kutoa wito kwa wanaotarajia kushiriki mbio na tamasha hilo kujiandikisha.Mkuu wa Wilaya ya Mwanga Bi, Mwanahamisi A. Munkunda, akizungumza na waandishi wa habari hawapo katika picha juu ya mbio za Mwanga  Festival Marathon zitakazo fanyika Desemba 27, mwaka huu wilayani humo. 

Katibu wa Kamati ya Maandalizi ya matukio hayo Bi. Zawadi Mirambo, akizungumzia maandalizi ya mbio hizo na Tamasha la Utalii.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.