Kidumo; awaongoza wakazi wa njoro kujiandikisha Daftari la Wakazi

 

Mstahiki Meya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi Mhandisi Zuberi Abdalaah Kidumo, akijiandikisha kwenye daftari la Mkazi 

MOSHI-MANISPAA

Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Moshi Mhandisi Zuberi Abdallah Kidumo,  amewaongoza Wakazi wa Kata ya Njoro, kujiandikisha katika Daftari la mpiga Kura kwa ajili ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, huku akiwataka kuendelea kujitokeza kushiriki zoezi hilo ili kujihakikishia haki yao kikatiba ya kushiriki katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu mwaka 2025.

Zoezi la kujiandikisha katika Daftari la Mpiga kura lilianza Oktoba 11, 2024 kwa nchi nzina na linatarajiwa kufika ukomo wake Oktoba 20, mwaka huu.

Akiwa kwenye Kituo cha mpiga kura Njoro mtaa wa Dobi Mstahiki Meya Kidumo, amekuwa ni miongoni mwa wakazi wa kata hiyo, waliojiandikisha na baadae akawaasa wakazi wa kata hiyo kulichukulia jambo hilo kwa umakini mkubwa.

“Niwaombe sana wakazi wa Manispaa ya Moshi kwa ujumla, kujitokeza kwa siku hizi zilizopangwa na (TAMISEMI) ili kuweza kujiandikisha kutoka Oktoba 11, mpaka Oktoba 20, 2024 ambapo mkishajiandikisha katika Daftari la Mkazi, maana yake ndio mtakuwa mmepata tiketi halali ya kuweza kuwa wapiga kura halali mwezi Novemba 27, 2024 .”amesema Mhandisi Kidumo.

Mstahiki Meya huyo amesema kuwa Wananchi wanaostahili kushiriki uchaguzi huo ni Watanzania wenye umri wa kuanzia miaka 18 na kuendelea, wenye akili timamu na ambao hawatumikii kifungo gerezani.

Amesema viongozi watakaochaguliwa katika uchaguzi huo ni Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji na Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji ambao jumla yao watakuwa si chini ya 15 na hawatazidi 25.

Katika ngazi ya mtaa, Kidumo amesema Wakazi wa mtaa husika watamchagua Mwenyekiti na Wajumbe wa Kamati ya mtaa,  jumla ya viongozi wote watakuwa watatu, na hawatazidi watano.

Aidha amesema katika ngazi za vitongoji  wakazi wote wa kijiji husika wenye sifa ya kupiga kura  watawachagua Wenyeviti wa vitongoji vyote vya kijiji hicho ambao kiutawala watakuwa sehemu ya uongozi wa kijiji husika.

Pia amesisitiza kwamba yeyote ambaye hatajiandikisha katika Daftari la Wakazi hatakuwa na haki ya kuwachagua viongozi wala kuchaguliwa kuwa viongozi katika ngazi husika.

Ameongeza kuwa masharti kwa wenye nia ya kugombea nafasi yoyote ya uongozi katika uchaguzi huo ni raia wa Tanzania, wakazi wa eneo husika, walioteuliwa na chama cha siasa chenye usajili wa kudumu.

Vilevile amesema kuwa wagombewa watatakiwa kuwa wanaojua kusoma na kuandika kwa lugha ya kiswahili au kiingereza, wenye umri usiopungua miaka 21, wenye akili timamu na ambao hawatumikii kifungo gerezani.



Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.