Kahawa Marathon kuanza Kilimanjaro

Mkuu wa Wilaya ya Moshi James Kaji, akikata utepe kuashiria ufunguzi wa Kahawa Festival-2024, msimu wa Tano, Septemba 4,2024 hafla iliyofanyika katika Kiwanda cha kukoboa Kahawa cha Tanganyika Coffee Curing kilichopo mjini Moshi mkoani humo.

MOSHI-KILIMANJARO

Wadau wa Kahawa Mkoani Kilimanjaro wametakiwa kuanzisha mashindano ya Kahawa Marathon ili kuongeza unywaji wa kahawa ya ndani kutoka asilimia 7 hadi kufikia asilimia 15 ifikapo mwaka 2025.

Mkuu wa Wilaya ya Moshi James Kaji, ameyasema hayo mnamo Septemba 4,2024 wakati wa ufunguzi wa  Tamasha la Tano la Kahawa “Kahawa Festival-2024,”  ufunguzi uliofanyika katika kiwanda cha kukoboa Kahawa cha Tanganyika Coffee Curing kilichopo mjini Moshi mkoani humo.

Amesema kuanzishwa shindano hilo la Kahawa Marathon litakuwa ni hatua muhimu katika kuimarisha utamaduni wa kahawa nchini na kutoa fursa za kiuchumi kwa wazalishaji wa kahawa.

Amesema uanzishwaji wa mashindano hayo ya ‘Kahawa Marathon’ yataleta mabadiliko makubwa katika unywaji wa kahawa ya ndani na hivyo kuongeza kiwango cha unywaji wa kahawa kutoka asilimia 7 ya sasa hadi kufikia asilimia 15 ifikapo mwaka 2025.

Amesema kuanzishwa kwa mashindano hayo yataweza kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa unywaji wa kahawa kama kinywaji cha afya na tamaduni na kwamba mashindano ya Kahawa Marathon si tu yatakuwa fursa ya burudani, bali pia ni jukwaa la kuelimisha watu kuhusu faida za kahawa," amesema.

"Tunataka kahawa kuwa sehemu ya maisha ya kila siku kwa kuanzisha mashindano haya ya ‘Kahawaa Marathoni’ yatakwenda kuleta burudani na elimu kwa wakati mmoja," amesema DC Kaji.

Mkuu huyo wa Wilaya amesema pamoja na kuhamasisha unywaji wa kahawa wa ndani, mashindano ya Kahawa Marathon yanaweza pia kusaidia kuongeza mapato kwa jamii, kuvutia washiriki na watalii na yataweza pia kutoa fursa za kibiashara zinazohusiana na zao la kahawa na hivyo kukuza uchumi wa eneo hilo.

Awali Mwenyekiti wa Kahawa Festival 2024, Denis Mahulu, amesema idadi ya watu wanaoshiriki kuonyesha bidhaa zinazotokana na zao la kahawa inazidi kuongezeka kila mwaka ambapo washiriki kutoka maeneo mbalimbali, wamekuwa wakishiriki kuonyesha ubunifu na ubora katika bidhaa zao.

Mahulu amesema kwamba ongezeko la washiriki hao ni dalili nzuri ya ukuaji wa sekta ya kahawa, kupitia Tamasha la Kahawa Festival-2024, wakati tamasha hilo  linaanzishwa mwaka 2019 washiri walikuwa 25 na kwa sasa washiriki wako zaidi ya 40, ambapo tamasha hilo, linatoa fursa kwa wakulima na wazalishaji wa kahawa kuungana, kubadilishana mawazo, na kujifunza mbinu bora za kilimo na usindikaji.

"Hii ni nafasi nzuri kwa wakulima kuja kujifunza jinsi ya kuongeza thamani ya bidhaa zao na kufikia masoko mapya," amesema.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Bodi ya Kahawa Tanzania (TCB), Primus Kimaryo, amesisitiza umuhimu wa matamasha ya kahawa katika kusaidia wakulima wa zao hilo kupata mbinu bora za kilimo.

Amesema kuwa Tamasha la Kahawa Festival-2024, linatoa jukwaa kwa wakulima kukutana na wataalamu wa kilimo, ambapo wanaweza kupata mafunzo kuhusu mbinu za kisasa za kilimo, usimamizi wa mashamba, na teknolojia mpya.

"Tunaamini kuwa elimu hii ni msingi wa maendeleo. Wakulima wanapojifunza mbinu bora, wanakuwa na uwezo wa kuongeza uzalishaji na kuboresha ubora wa kahawa yao," amesema Kimaryo.

Kimaryo ameongeza kuwa matamasha yanaweza kusaidia kuboresha soko la kahawa nchini, kwa kutoa elimu na mafunzo, wakulima wataweza kuzalisha kahawa bora, ambayo itavutia wanunuzi na kuongeza thamani ya bidhaa za wakulima wa zao hilo katika masoko ya ndani na nje.

Kauli Mbiu ya Kahawa Festival 2024 inasema; “Ushirikiano wa dau kwa Pamoja katika uendelezaji wa tasnia ya Kahawa.”

 






Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.