Ujenzi wa Makazi ya watu kumefanya uzalishaji wa zao la Kahawa kuzorota

 

NA KIJA ELIAS, MOSHI.

Kuzorota kwa uzalishaji wa kahawa katika mikoa ya kanda ya kaskazini, kumetajwa kuchagizwa na sababu mbalimbali, ikiwemo kwa baadhi ya wakulima kubadili matumizi ya ardhi ya kilimo kwa kujenga makazi ya kuishi.

Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro Nurdin Babu, ameyasema hayo Septemba 9,2024  wakati  wa hafla fupi ya ufunguzi rasimi wa maandalizi ya tamasha la msimu wa Tano wa Kahawa Festival 2024, uliofanyika katika  ukumbi wa mikutano wa Bodi ya Kahawa nchini TCB mjini Moshi.

Amesema kubadilishwa kwa matumizi ya ardhi ya kilimo cha kahawa kwa mikoa ya kanda ya Kaskazini kwa ajili ya makazi na shughuli zinginezo kusababisha kushuka kwa uzalishaji wa zao hilo.

”Watu wanabadilisha maeneo ya kilimo cha kahawa na kujenga nyumba za makazi, nitoe wito kwa watu wanaotaka kujenga makazi ya kuishi ni vizuri wakaenda kujenge kwenye maeneo ya tambarare, maeneo ya mlimani ambako zao la kahawa hustawi vizuri wakayacha kwa ajilia ya shuhughuli za kilimo cha kahawa,”amesema RC Babu.

Aidha amesema kuweko kwa mabadiliko ya tabia nchi, mtawanyiko wa mvua, vipindi virefu vya ukame kwenye maeneo yanayolima kahawa na matumizi duni ya pembejeo hususani mbolea za viwandani yamesababisha pia kushuka kwa tija ya uzalishaji wa kahawa.

Amesema sababu nyingi ambayo inasababisha kushuka kwa kiwango cha uzalishaji wa zao hilo ni pamoja na kuyumba kwa bei ya zao kahawa duniani na hivyo kuathiri mipango ya wakulima katika kuendeleza zao hilo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Bodi ya Kahawa Tanzania (TCB), Primus Kimaryo, amesema unywaji wa kahawa nchini umekuwa ukisuasua licha ya utengenezaji mzuri wa kinywaji hicho.

“Tanzania tunalima Kahawa, asilimia 93 inakwenda nje, lakini unywaji wetu bado unasuasua kwa asilimia 7, ukipita leo mahotelini kote wanako lala wageni, licha ya Tanzania kuwa mzalishaji mzuri sana wa kahawa, bado kahawa inayonywewa na wageni haitoi taswira kwamba tunatengeneza kahawa nzuri kiasi hicho,” amesema Kimaryo.

Awali akizungumza Mwenyekiti wa Kahawa Festival 2024 Denis Mahulu, amesema  ili kupata maendeleo endelevu, kuna haja ya wadau wa Kahawa kushirikiana kwa pamoja ili kuweza kuleta maendeleo endelevu katika mnyororo mzima wa thamani wa kahawa.

“Mnyororo unaanzia kwa mkulima, wachakataji kuanzia ngazi ya awali, watoa huduma mbalimbali, wakiwemo wale wa pembejeo, elimu, utafiti, wasimamizi wa zao la kahawa, pamoja na wanunuzi wa ndani na nje ya nchi”,amesema Mahulu.

Mwenyekiti huyo amesema namna pekee ya kuongeza unywaji wa ndani wa kahawa ni kupitia tamasha kama hilo.

“Unywaji wa kahawa wa ndani bado uko chini, mkakati wetu ni kupitia tamasha hili (Kahawa Fetival-2024) litakwenda kuongeza unywaji wa kahawa kutoka asilimia 7 hadi kufikia asilimia 15,”amesema.

Aidha amesema kuwa tamasha hilo ambalo hufanyika kila mwaka Oktoba mosi ambayo huwa ni siku ya Kahawa duniani,  na kwamba mwaka 2024 litafanyika kwa siku tatu mfululizo ili kuhamasisha soko la ndani kwa Watanzania.

“Inatuhitaji sote tushirikiane katika kuongeza thamani ya zao la kahawa, ili kuweza kufikia lengo hilo ni pamoja na matamasha kama haya,” amesema Denis Mahulu, Mwenyekiti wa Kahawa Festival 2024. 

Mada mbalimbali zitawasilishwa ikiwemo faida ya unywaji wa kahawa, kwendana na masoko ya kahawa, matumizi ya pembejeo, matokeo yaliyofanywa na TaCRI.

Utengenezaji wa kahawa, uonjaji wa kahawa , kushindanisha kahawa ili kuweza kupata kahawa bora ya kahawa.

Kauli Mbiu ya Mwaka huu; Ushirikiano wa dau kwa Pamoja katika uendelezaji wa tasnia ya Kahawa.



Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.