Maabara za ubora wa maji ni
eneo muhimu katika kuhakikisha huduma ya maji wanayopatiwa wananchi inakuwa
salama kwa matumizi yao.
Serikali kupitia Wizara ya
Maji, ndio inayosimamia maabara za maji kwa nchi nzima ambazo, zimegawanyika
katika mikoa mbalimbali.
Akitoa taarifa ya
utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa Maabara ya ubora wa Maji kwa Kamati ya Siasa
mkoa wa Kilimanjaro Mkurugenzi wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira
Mjini Moshi Mhandisi Kija Limbe amesema (MUWSA) ilianza utekelezaji wa ujenzi
wa maabara hiyo Agosti 2024 na kukamilika Aprili, 2024.
Mhandisi Limbe amesema
awali mamlaka hiyo, ilikuwa na maabara ndogo kwa ajili ya ubora wa Majisafi, kutokana
na Mamlaka hiyo kuongezewa maeneo ya kutoa huduma , waliamua kubuni mradi wa
ujenzi wa maabara kubwa itakayokidhi mahitaji yanayoendana na ongezeko hilo.
“Zaidi ya wateja 58,246 wanaoishi
katika Manispaa ya Moshi na maeneo ya Moshi Vijijini yanayo hudumiwa na MUWSA,
hivyo tuna hakikisha wateja wote hawa wanapata huduma ya majisafi na salama kwa
ajili ya kuboresha afya zao,” amesema.
Amesema mradi huo mpaka
kukamilika kwake umegharimu kiasi cha Sh milioni 81.8 inayojumuisha gharama za
ujenzi wa jengo pamoja na ununuzi wa vifaa vya maabara na fedha hizo ambazo zimetumika
kugharamia ujenzi wa maabara hiyo ni fedha kutoka mapato ya ndani.
“Utekelezaji wa mradi huu umekamilika kwa asilimia 100, ikiwemo ujenzi wa jengo la maabara, ujenzi wa mtaro wa kudhibiti maji ya mvua na ufungaji wa vifaa vya maabara na kwamba Mamlaka hiyo iko kwenye mchakato wa kuendelea kununua vifaa vingine vya maabara,”amesema Mhandisi Limbe.
Mwenyekiti wa CCM MKoa wa Kilimanjaro
Patrick Boisafi, amempongeza Mkurugenzi wa (MUWSA) na timu yake kwa kubuni
mradi huo ambao utakwenda kuwanufaisha wananchi wa Manispaa ya Moshi na maeneo
mengine kwa kupata huduma bora na endelevu ya Majisafi na salama.
Awali akizungumza Mstahiki
Meya wa Manispaa ya Moshi Injinia Zuberi Kidumo, amesema viko baadhi ya vijiji
bado vinatumia maji ya visima na kuiomba Mamlaka hiyo, kutoa elimu zaidi hususani
maeneo ya vijijini, kabla hawajaanza kuyatumia maji hayo wawze kuja kupima maji
hayo ili kujua usalama wake zaidi.
Naye Mbunge wa Jimbo la
Moshi Mjini Priscus Tarimo, amesema yako maeneo ambayo watu bado wanaharibu
mazingira kwa kuchota mchanga kwenye mito na kutoa mawe kwa ajili ya kuponda
kokoto na hivyo kusababisha vyanzo vya
maji kupungua.
“Niwaombe MUWSA badala ya
kuwafukuza kwa Sheria watu hao ni vizuri MUWSA ikawatafutia shughuli mbadala kwa
kutumia CSR inayopatikana kwenye mamlaka hiyo ili waweze kuondokana na
uharibifu huo wa kimazingira kwenye mito,”amesema Mbunge Tarimo.
Akitoa maelezo ya namna
maabara hiyo inavyofanya kazi Fundi sanifu Mwandamizi kutoka MUWSA Joseph
Revocatus, amesema maabara ya ubora wa maji ni maabara maalumu ya kupima maji
ili kuona kemikali zilizopo ambazo zinaweza kuzidi au kupungua kukawa na
madhara kwa binadamu pamoja na viumbe hai kwenye mwili wa binadamu.
“Maabara hii inauwezo wa kuchukua
sampuli zisizo pungua 56, ingawa tumejiwekea kuchukua vipimo vya sampuri 48,
ambapo tumeweka vituo kwenye maeneo yote ambayo tunayahudumia, ikiwemo kwenye
taasisi za elimu, vilula, masoko, vyanzo vya maji na kwenye matanki ili kujua
ubora huo wa maji,”amesema mtaalamu huyo wa maabara ya ubora wa maji.
Kwa upande wake Mkuu wa
Mkoa wa Kilimanjaro Nurdin Babu, ameupongeza uongozi wa MUWSA kwa kufanya utafiti ambao umewezesha kujenga maabara hiyo ya ubora
wa maji.
Mamlaka ya Majisafi na
Usafi wa Mazingira MUWSA ndio Mamlaka bora Tanzania kwa miaka mingi inaongoza
kwa kutoa huduma bora za maji.