Manispaa ya Moshi yatangaza majina ya mipaka ya Mitaa Uchaguzi Serikali za Mitaa



MOSHI-KILIMANJARO.

Halmashauri ya Manispaa ya Moshi, Mkoa wa Kilimanjaro, imetangaza majina na mipaka ya mitaa iliyoko katika Manispaa hiyo, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika Novemba 27 mwaka 2024.

Akitoa tangazo hilo Septemba 16, 2024, wakati akizungumza na viongozi mbalimbali walioshiriki katika kikao hicho kilichofanyika ukumbi wa mikutano wa halmashauri hiyo na kuhudhuriwa na Mstahiki Meya Mhandisi Abdallah Kidumo, Mbunge wa Jimbo la Moshi Mjini, Madiwani, Viongozi wa vyama vya Siasa, Wataalamu wa halmashauri pamoja na Watendaji wa Kata na Mitaa.

Msimamizi wa uchaguzi huo Mwl. Mwajuma Nasombe, ametumia fursa hiyo kuwataka Watendaji wa Mitaa kuwa mabalozi wazuri wa kufikisha taarifa mbalimbali za uchaguzi ikiwa ni pamoja na elimu ya uraia kwa kutoa matangazo kwa njia mbalimbali katika maeneo yao.

“Ni haki ya wananchi kupata taarifa zote za uchaguzi kwa wakati na kwa uwazi mkubwa ili kufanya uamuzi sahihi katika kuchagua viongozi wanaowataka, hivyo ni jukumu lenu watendaji kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi.”amesema Mwl. Nasombe.

Msimamizi huyo wa uchaguzi, ametumia fursa hiyo kuwataka viongozi wa Serikali za Mtaa kushirikiana kwa pamoja kuweza kuwabaini wale wote wenye sifa ambao watakuwa na haki ya kujiandikisha ili kuepusha kuandikisha mamluki.

“Oktoba 21 mpaka 27 mwaka huu, kutakuwa na ukaguzi wa orodha ya wapiga kura, msimamizi wa uchaguzi ana wajibu wa kubandika orodha ya wapiga kura ili kutoa fursa kwa wananchi waliojiandikisha kuhakiki majina yao ili kupata fursa ya kutumia haki yao ya kimokrasia,”amesema Mwl. Nasomnbe.

“Novemba Mosi hadi Novemba 7 mwaka huu litakuwa ni zoezi la kuchukua na kurudisha fomu za kugombea, hivyo niwaombe Watanzania wote wenye sifa za kugombea wajitokeza kwa wingi ili kuweza kupata fursa ya kugombea pale ambapo watakuwa wamekidhi vigezo.

Amesema Novemba 1 hadi 7 itakuwa ni siku ya kuchukua fomu na kuirejesha  na Novemba 8 itafiuata ratiba ya uteuzi ya wagombea na baada ya hapo Novemba 20 mpaka novemba 26 mwaka 2024 wale wote ambao watakuwa wamepewa dhamana na kuteuliwa wanahaki ya kufanya kampeni na Novemba 27 itakuwa ni siku ya kufanya uchaguzi.

Vile vile amesema kuwa Novemba 11 mpaka 20 mwaka huu itakuwa siku ya wananchi kujitokeza kujiandikisha kwenye daftari la mkazi, huku akisema kuwa ni wajibu watendaji hao kuwakumbusha wananchi mwenye sifa za kujiandikisha waweze kujitokeza kujiandikisha.

“Mwananchi mwenye sifa za kujiandikisha kwenye daftari la mkani ni yule ambaye atakuwa na sifa nne kwa anatakiwa kuwa  raia wa Tanzania, awe na akili timamu, awe mwenye na umri kuanzia miaka 18, lakini pia  lazima awe mkazi wa mtaa husika.”amefafanua.

Aidha ametumia fursa hiyo kuwataka viongozi wote wa Serikali za Mtaa walioko madarakani ifikapo Oktoba 25 mwaka huu, watakuwa na wajibu wa kuzirudisha nyaraka zote za Serikali  ambazo walikabidhiwa kwa sababu uongozi wao utakuwa umefika ukomo.

Uchaguzi wa Serikali za Mitaa hufanyika kila baada ya miaka mitano, kwa kuzingatia matakwa ya Sheria ya Serikali za Mitaa, Mamlaka za Mitaa sura 287 na Sheria za Mitaa ya Mamlaka za Mji sura 28, ambapo wananchi hutumia haki yao ya kikatiba kuomba kuongoza wenzao na kuchagua viongozi katika maeneo wanayoishi.

Uchaguzi utakaofanyika Novemba 27 mwaka 2024, utakuwa ni wa saba tangu mfumo wa vyama vingi vya siasa kuingia nchini mwaka 1992.














Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.