MOSHI-KILIMANJARO
Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Moshi Mwl. Mwajuma Nasombe, amewataka
wakazi wa Manispaa hiyo, kujitokeza kwa wingi kushiriki uchaguzi wa Serikali za
Mitaa unaotarajia kufanyika Novemba 27, 2024.
Wito huo umetolewa jana Septemba 28,2024 wakati akizungumza na wakazi
wa Manispaa hiyo waliojitokeza kuangalia bonanza kati ya timu ya Umoja wa Bajaj
na Bodaboda waliocheza na timu ya Watumishi wa Manispaa hiyo, bonanza lililokuwa
limelenga kuhamasisha Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2024 lililoandaliwa na
Manispaa hiyo.
Nasombe
amesema kuwa ili mwananchi aweze kupiga kura siku ya Uchaguzi wa Serikali za
Mitaa, anapaswa kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la mpiga kura, ambapo
zoezi la uandikishaji litafanyika kuanzia Octoba 11 hadi 20, 2024.
“Mwaka
huu tutakuwa na zoezi kubwa la Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, utakaofanyika
Novemba 27,2024, niwaombe Wakazi wa Manispaa ya Moshi, tujitokeze kwa wingi wetu
tushiriki uchaguzi huu kwa Maendeleo ya Kata zetu, usikubali mtu mwingine
akuchagulie kiongozi wakati una uwezo wa kupiga kura,” amesema Mwl. Nsombe.
Kwa
upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Kilimanjaro Kiseo Yusuf Nzowa, ametoa wito
kwa wananchi wote wa mkoa huo, kujitokeza kushiriki uchaguzi huo wa Serikali za
Mitaa.
“Nikupongeze
sana Mkurugenzi Mwajuma Nasombe kwa ubunifu wako huu na kuweza kuandaa bonanza
hili la michezo mbalimbali kama sehemu ya hamasa kuelekea Uchaguzi wa Serikali
za Mitaa ambao utafanyika Novemba 27, 2024,”amesema Nzowa.
Akizungumza
Msimamizi msaidizi wa uchaguzi Manispaa ya Moshi Denis Robert Shette, amesema kabla
ya kuanza kwa bonanza hilo, halmashauri ya Manispaa ya Moshi iliandaa
maandamano ambayo yalianzia katika ofisi za Manispaa, kupitia Stendi kuu ya mabasi
hadi katika Uwanja wa mpira Majengo, ambako bonanza hilo lilipofanyikia.
Amesema
bonanza hilo,
lilihusisha mpira wa wavu, kwa timu ya Wanawake kutoka Chuo Kikuu cha Ushirika
Moshi (MoCU) ambayo ilicheza na timu ya Wanawake ya Manispaa ya Moshi.
Shette amesema michezo mingine iliyofanyika katika uwanja huo ni pamoja na mashindano
ya kunywa soda na mchezo wa ngumi uliohusisha mabondia kutoka Chama cha Ngumi Mkoani
Kilimanjaro.