Watendaji Same waonywa kutozigeuza pikipiki kuwa bodaboda


                                  SAME-KILIMANJARO

Halmashauri ya Wilaya ya same imekabidhi pikipiki kwa watendaji wa kata ili kuwarahisishia ukusanyaji wa mapato, huku ikiwaonya watendaji hao kutozigeuza pikipiki hizo kuwa bodaboda.

Onyo hilo limetolewa Agosti 28,2024 na Mwenyekiti wa Halmashari hiyo Yusto Mapande, wakati akikabidhi pikipiki hizo  kwa maofisa watendaji wa kata tatu za Miamba, Chome na Vudee  ambazo ziko ukanda wa milimani.

Amesema kuwa pikipiki hizo ambazo zimegaiwa ni mali ya Halmashauri hivyo mtendaji yeyote akipatikana anafanya biashara ya bodaboda  tofauti na matumizi ambayo yamekusudiwa hawatasita kuzichukua na kuzipeleka sehemu nyingine  kwa watendaji wa kata ambao hawana usafiri huo.

“Watendaji wa kata tuliowakabidhi pikipiki hizi hakikisheni mnavitumia vyombo hivi kwa malengo yaliyokusudiwa na wale ambao watakwenda kinyume tutawanyang’anya pikipiki hizi na kuwapa watendaji wengine wenye uhitaji,”amesema Mapande.

Amesema pikipiki hizo wamezikabidhi kwa watendaji kwa lengo la kwenda kuongeza kasi ya ukusayaji wa mapato na usimamizi wa miradi ya maendeleo pamoja na kuongeza uwajibikaji kwa kutatua kero mbalimbali wananchi kwenye kata zao.

Akizungumza  kwa niaba ya mtendaji kata ya Miamba Diwani wa Kata hiyo Greyson Kiondo Fue, ameishukuru Halmashauri hiyo kwa kuwagaiwia pikipiki hizo jambo ambalo litawasaidia katika utekelezaji wa majukumu yao.

“Tunaishukuru sana serikali imetusaidia kutuwezesha nyenzo muhimu ya usafiri wa pikipiki kwasababu awali tulikuwa tunapata changamoto kubwa ya umbali wa maeneo katika ukusanyaji wa mapato pamoja na ufuatiliaji wa miradi kutokana na jiografia ya maeneo yetu ya milimani,”amesema.

Kwa upande wake Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM Wilaya ya Same Amosi Kusakula, amesisitiza Watendaji kuhakikisha wanakwenda kutatua kero za wananchi.

“Changamoto na migogoro mingi inayotokea, mingi inasababishwa na baadhi ya uzembe wa watendaji ndani ya serikali, sisi kama viongozi wa chama ni vizuri tukaiambi

Aidha amesema viongozi wa serikali kuwajibika kwenye chama tawala si hisani bali ni matakwa ya kikatiba, hivyo wanao wajibu wa kutoka ofisini na kwenda kutatua changamoto za wananchi na waondoe dhana kwamba hiyo ni kazi ya vyama vya siasa.

MWISHO.







 

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.