Kamisaa wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na Mkuu wa Mkoa wa
Kilimanjaro Nurdin Babu, amesema mshikamano ndio nyenyo muhimu ya
ushindi kwa chama hicho na kamwe kama wanachama wa CCM watashirikiana na
viongozi wao walioko madarakani hawawezi kupata ushindi.
Akizungumza
Julai 18,2024 na Viongozi wa CCM wa ngazi mbalimbali, kuanzia mashina,
matawi, kata hadi wilaya, kwenye ufunguzi wa semina elekezi,
iliyoandaliwa na CCM Wilaya ya Moshi MJini, mkutano ambao uliofanyika
kwenye ukumbi wa mikutano wa CCM mkoani humo.
Amesema
hakuna kitu kizuri katika shughuli za kisiasa kama kuwa na ushirikiano
mzuri kwa viongozi na wanachama ili kuendelea kushika dola.
Amesema
kutokuwa na ushirikiano huibua migogoro , jambo ambalo amesema
halitarajii kulisikia na kuwataka viongozi na wanachama kuwa wamoja.
“Mshikamano
ndani ya CCM, ndio nyenzo ya kwanza kwenye chama, kama Wanachama
hawatashirikiana na viongozi wao ambao watakwenda kugombea nafasi
mbalimbali za uongozi kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa
kufanyika mwaka huu, hawawezi kupata ushindi wa CCM,” amesema.
Aidha
amempongeza Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Moshi Mjini na Kamati yake ya
Siasa, kwa maamuzi mazuri kwa kuwa wilaya ya kwanza kutoa semina hiyo
kwa viongozi mbalimbali wakiwemo mabalozi.
Mwenyekiti
wa CCM Wilaya ya Moshi Mjini Faraji Swai, amesema semina hiyo, imelenga
kuwajengea uwezo viongozi hao, ili watakapokwenda kwenye uchaguzi wa
Serikali za Mitaa yako mambo ambayo wanapaswa kuyafuata pasipo kuvunja
kanuni za uchaguzi.
Awali
akizungumza Katibu wa CCM Wilaya ya Moshi Mjini Frida Kaaya, amesema
katika kuelekea kwenye uchaguzi amewasihi wajumbe hao kuwa kitu kimoja
ili kukiletea ushindi chama hicho.
Naye
Mbunge wa Jimbo la Moshi Mjini Priscus Tarimo, amesema katika ahadi
zake 10 ambazo, aliziahidi kwa wananchi, wakati wa kampeni za uchaguzi
mwaka 2020 nyingi zinaendelea kutekelezwa ikiwemo ukarabati wa uwanja wa
Ndege Moshi, Ujenzi wa hospitali ya Wilaya na nyingine nyingi.
Amesema
katika sekta ya elimu, Tarimo amesema zaidi ya madarasa 300 yamejengwa
kwenye shule za msingi na sekondari, sanjari na ujenzi wa shule mpya za
sekondari kwenye kata ambazi zilikuwa hazina sekondari.