T.A.G Gethsemane Hai yapongezwa malezi ya Watoto

 

BOMANG’OMBE, HAI

Serikali imelipongeza Kanisa la Tanzania Assemblies Of God (TAG) Gethsemane lililopo Wilayani Hai mkoani Kilimanjaro kwa namna ambavyo linawajengea watoto wadogo misingi mizuri ya kumjua Mungu.

Mkuu wa Wilaya ya  Hai Amiri Mkalipa, alitoa pongezi hizo wakati akitoa salamu za Serikali kwenye maadhimisho ya miaka 85 ya kuanzishwa kwa Kanisa la Tanzania  Assemblies Of God (TAG) hapa nchini.

Hafla ambayo ilienda sambamba na maadhimisho ya kutimiza miaka 44 ya kuanzishwa kwa Kanisa TAG Gethsemane lililopo Wilayani humo.

Amesema mambo ambayo yamemfurahisha wakati amefika kanisani hapo ni namna ambavyo Kanisa la TAG  linavyowajengea misingi ya kuwaandaa watoto wadogo kuja kuwa Watanzania waliobora na hivyo akawataka wazazi na walezi kuendelea kuwalea watoto wao katika misingi ya dini, Ili kutengeneza kizazi chenye hofu ya Mungu.

Amesema mzazi bora ni yule anayemchukua mtoto wake na kwenda naye kanisani kwani atajua madhara ya ukatili wa kijinsia pamoja na madhara ya ulawiti.

Aidha mkuu wa wilaya ya Hai, amelipongeza kanisa la TAG kwa na utaratibu wa kujitolea na kwenda kuwasaidia watoto wenye mahitaji maalum ili kueneza upendo kwa wasio na uwezo kujiona wako, sanjari na kushiriki shughuli za m upandaji wa miti pamoja na uchangiaji wa damu.

Awali akizungumza mzee Kiongozi wa Kanisa la TAG  Gethsemane Wilaya ya Hai, Daudi Lekei, amesema katika kuadhimisha miaka 85 ya TAG  nchini, wameshiriki  upandaji wa miti,  kufanya usafi wa mazingira katika maeneo yanayozunguka kanisa, kuchangia damu pamoja na kwenda kutembelea kituo cha watoto yatima na kutoa misaada mbalimbali ya kibinadamu.

Maadhimisho ya miaka 85 ya kuanzishwa kwa TAG hapa nchini ni kufuata maandiko matakatifu ya Mungu ya kukumbuka na kuyaishi mambo mazuri ya watangulizi katika kuongoza kondoo wa Bwana.

 

 

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.