Maofisa 237 Jeshi la Magereza Kanda ya Kaskazini watunukiwa nishani



GEREZA LA KARANGA, MOSHI

Maofisa na Askari wa Jeshi la Magereza Kanda ya Kaskazini 237 wamevalishwa Nishani walizotunukiwa na Rais Samia Suluhu Hassan katika kuadhimisha miaka 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Akizungumza kwenye tukio la hilo Kamishna Jenereli wa Jeshi la Magereza nchini (CGP)Mzee Nyamka amesema idadi hiyo inayojumuisha Makao Mkuu ya Jeshi la Magereza nchini lina maofisa na Askari takribani 15,000.

"Utaona siyo wote waliotunukiwa ni wachache na hawa wamejipambanua kutokana na hao wengine kuwa na nidhamu , maadili mema na utendaji wa kupigiwa mfano.” amesema CGP Nyamka

 Amesema kwa wale ambao hawajabahatika kutunukiwa itakuwa ni chachu ya kuwafanya wazidishe juhudi kwenye utendaji wao kwa kuzingatia nidhamu, sheria kanuni na taratibu ili awamu ijayo rais samia atakapotunuku nishani na wao wawe miongoni mwao.

Akizungumzia suala la upandaji miti ndani ya jeshi hilo, (CGP) Nyamka, amesema jeshi hilo lina kampeni maalum ya  upandaji wa miti ikiwa ni kuitikia na kutekeleza maagizo ya wakuu wa nchi, ambayo wamekuwa wakiyasisitiza kuhusiana na utunzaji wa mazingira.

“Malengo ya jeshi la Magereza nchini ni kupanda miti isiyopungua milioni 1.5, ambapo hadi sasa zaidi ya asilimia 50 ya malengo tarajiwa tumekwisha kuyafikia katika zoezi la upandaji wa miti ndani ya jeshi letu”,.

Ameongeza kuwa mazingira yasipotunzwa na kulindwa zipo athari kubwa ambazo kama nchi imekuwa ikizishuhudia hivi karibuni ikiwemo mabadiliko ya tabia nchi na mafuriko, ambayo yote hayo yanachangiwa na shughuli za kibinadamu.

Nao baadhi wa maofisa waliovishwa nishani hiyo akiwemo Mkuu wa Gereza la  Loliondo  Wilaya ya Ngorongoro Mrakibu George Sosindi na Mkuu wa Gereza la Mkoa wa Tanga Upendo Kazumba, wamemshukuru Rais Samia kwa kuweza kupata fursa ya kuwa miongoni mwa maofisa wachache wa jeshi la magereza kuweza kuvishwa nishani hizo.





Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.