Manispaa ya Moshi yashika nafasi ya Pili Tuzo za Wizara ya Afya

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Moshi Injinia Zuberi Kidumo akipokea Tuzo ya Afya na Usafi wa Mazingira kutoka kwa Waziri wa Afya Ummy Mwalimu katika Hafla iliyofanyika Kibaha, Pwani leo Mei 10, 2024 ambapo Manispaa ya Moshi imeshika nafasi ya pili nchini. (Picha na KISENA)

KIBAHA, PWANI

Manispaa ya Moshi imeshika nafasi ya pili nchini Tanzania katika tuzo za Halmashauri bora katika Afya na Usafi wa Mazingira inayotolewa na Wizara ya Afya ili kuongeza tija na ushindani kwa maendeleo ya taifa kwa ujumla.

Akizungumza baada ya kukabidhiwa tuzo hiyo Mstahiki Meya wa Manispaa ya Moshi Injinia Zuberi Kidumo amesema mwaka huu wamepanda nafasi moja baada ya mwaka 2022-2023 kushika nafasi ya tatu

“Tunashukuru sana kwa kupata nafasi hii ya kuwa washindi wa pili hizi ni jitihada kubwa mwaka jana Manispaa ya Moshi tulikuwa washindi wa nafasi ya tatu na mwaka huu tumesogea na kuwa washindi wa pili,” amesema Injinia Kidumo.

Manispaa ya Moshi ni miongoni mwa Manispaa nchini ambazo zimekuwa katika kinyang’anyiro hicho kwa muda mrefu ambapo Injinia Kidumo ameweka bayana mikakati ya kuirudisha Moshi kuwa ya mfano katika kategori hiyo.

“Nafasi ya Kwanza imechukuliwa na Manispaa ya Shinyanga. Bado tunaendelea kupambana ili tuweze kushika katika nafasi ya kwanza kama zamani. Haya ni mashindano, sisi tukiwa tunapambana kuendeleea kutetea nafasi yetu ukae ukijua kwamba kuna mwenzako naye anapambana kuitaka hiyo nafassi ya kwanza anaboresha kwake,” ameongeza Mstahiki Meya huyo.

“Mikakati; ni kuhakikisha tunakwenda kuboresha zaidi maeneo yetu, taka zinakuwa ni changamoto kubwa sana kutokana na kila siku ya mungu familia zinaongezeka , familia mpya maeneo”, amesema Injinia Kidumo

Makamu wa Rais Dk. Philip Isdori Mpango, ametoa tuzo hizo akiwa sambamba na Waziri wa Afya Ummy Mwalimu na kuwakabidhi Manispaa na Halmashauri washindi katika hafla iliyofanyika  Kibaha, mkoani Pwani.  

Kwa upande wa Halmashauri ya Moshi imejinyakulia tuzo ya hospitali ya bora baada ya Hospitali ya Kibosho kushika nafasi ya Pili kwa utoaji wa huduma kwa wagonjwa.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.