Kampuni ya uzalishaji sukari ya TPC Limited iliyoko Moshi, mkoani Kilimanjaro imetoa msaada wenye thamani ya shilingi mil. 12 kwa waathirika wa mafuriko yaliyotokea wilaya ya Moshi, mkoani humo wiki iliyopita.
Akikabidhi
msaada huo leo Aprili 30, 2024 kwa niaba ya uongozi wa kampuni hiyo, mwanasheria wa kampuni
hiyo David Shilatu alisema uongozi wa TPC umeguswa na athari
walizopata wananchi wa maeneo mbalimbali mkoani humo kufuatia mafuriko
yaliyotokana na mvua zinazoendelea kunyesha mkoani Kilimanjaro.
“Tumeguswa
sana na majanga yaliyowapata wenzetu wengine wakiwa wanatoka maeneo
ambayo kijiografia TPC Limited inafanya shughuli zake za kila siku”,
alisema.
Alisema
kuwa misaada iliyotolewa ni pamoja na magodoro 25, mablanketi 50, tani
moja ya sukari, sabubi za kufulia, unga kwa ajili ya chakula, mafuta ya
kupikia, maji safi na salama ya kunywa pamoja na chumvi.
Akipokea
msaada huo kwa niaba ya serikali, Mkuu wa Wilaya ya Moshi Zephania
Sumaye, aliushukuru uongozi wa TPC Ltd kwa misaada hiyo ambayo alisema
imekuja kwa wakati muafaka.
“Uhitaji
wa wenzetu waliokumbwa na janga hili kubwa ni mkubwa haswa ikitiliwa
maanani zaidi ya kaya 900 zenye watu Zaidi ya 4,000 zimepoteza mali
pamoja na kukosa makazi ya kuishi baada ya kuathiriwa na mafuriko
makubwa yaliyotokea”, alisema.
“Ninakuweko
hapa kwenye kambi hii ambayo inayowahifadhi wahanga wa mafuriko haya
tangu yalipotokea; kuweko kwangu hapa kunanipa fursa ya kuona uhalisia
na ukubwa wa uhitaji wa waathirika hawa kufuatia athari walizopata”,
alisema na kuongeza, misaada waliyotoa TPC Ltd ni faraja kubwa kwa
waathirika wa mafuriko hayo.
Aidha
alisema serikali inaendelea na juhudi mbalimbali zinazolenga
kurekebisha miundombinu mbalimbali iliyoharibiwa maeneo mbalimbali
wilayani Moshi tangu kutokea mafuriko hayo.
“Tayari
miichakato imeanza inayolenga kuhakikisha hali inarudi kuwa nzuri kwa
wananchi walioathiriwa na mafuriko hayo; pia Tanroads na Tarura wameanza
kuondoa vifusi vilivyoko maeneo yaliyoathiriwa na mafuriko hayo ikiwemo
kwenye makazi ya watu”, alisema.