KATA TANO ZA MOSHI ZATAJWA KUKUBWA NA WIZI WA MITA ZA MAJI

MOSHI-KILIMANJARO.

Kata za Msaranga, Mwika Kusini, Rau, Mwika Kaskazini na Njiapanda zimeibuka kuwa miongoni mwa maeneo yanayoongoza kwa matukio ya wizi wa mita za maji katika eneo la Manispaa na wilaya  ya Moshi kwa ujumla, ambapo jumla ya mita 543 zenye thamani ya Sh milioni 65.1 zimeibiwa  ndani ya kipindi cha miaka mitatu iliyopita.

Taarifa hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Usambazaji Maji na Usimamizi wa Mazingira mjini Moshi (MUWSA), Mhandisi Innocent Lugodisha, wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana.

Kwa mujibu wa Mhandisi Lugodisha, alisema wimbi hilo la wizi limesababisha hasara kubwa kwa mamlaka hiyo na limekuwa likikwamisha juhudi za kuboresha huduma na miundombinu ya maji kwa wananchi.

“Mita hizi ni  ghali sana, kwani kila mita moja inauzwa Sh 120,000 na kama fedha zinazotumika kununua mita mpya zingetumika  kwenye miradi mingine ya maendeleo ya huduma ya maji, wananchi wangekuwa wamepata huduma bora zaidi kwa sasa,”alisema Mhandsi Lugodisha.

Aidha, alieleza kuwa kila inapong’olewa mita, maji huendelea kumwagika hovyo na kusababisha upotevu mkubwa, hasa  ikizingatiwa kuwa  tayari maji hayo hutibiwa kwa gharama kubwa kabla ya kufikishwa kwa mtumiaji wa mwisho.

“Tunapopoteza mita moja, si tu kwamba huduma ya maji inakatika kwa mwananchi, bali pia tunapoteza maji yaliyotibiwa kwa dawa, pamoja na nguvu kazi ya watumishi waliolipwa kuhakikisha maji yanawafikia wananchi,”aliongeza.

Mbali na mita, Mhandisi Lugodisha alibainisha kuwa pia kumekuwepo na wimbi la wizi wa mifuniko ya chemba, ambapo chemba 850 zimeibiwa kwa kipindi hicho na vifaa hivyo  kuuzwa kama vyuma chakavu kwa baadhi ya wafanyabiashara.

Alisema takribani Sh milioni 765, mamlaka imepata hasara kwa kuibiwa mifuniko ya chemba hizo, jambo ambalo limekuwa likirudisha nyuma jitihada za  kusambaza huduma hiyo ya maji.

“Tunaendelea kufuatilia kwa karibu wafanyabiashara wa vyuma chakavu, na yeyote atakayebainika kununua vifaa vya wizi, hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake,”alionya.

Aliongeza kuwa “Katika kukabiliana na tatizo hilo, MUWSA imechukua hatua ya kuanza kujenga chemba zenye ulinzi zaidi kwa mujibu wa Mhandisi Lugodisha, katika mwaka wa fedha 2024/2025 tayari chemba 350 zimejengwa  kwa ajili ya kulinda mita zaidi ya 2,000 na awamu ya pili itahusisha ujenzi wa chemba 500 kwa ulinzi wa mita zaidi ya 5,000.

Aidha alitoa wito kwa wananchi kuendelea kushirikiana na mamlaka kwa kutoa taarifa zitakazosaidia kukomesha wizi huo unaohatarisha ustawi wa huduma ya maji kwa jamii nzima.

Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa (MUWSA), Mhandisi Kija Limbe, alisema mpaka sasa mamlaka hiyo imepata hasara kubwa kutokana na wizi wa miundombinu hiyo.

“Wako baadhi ya wananchi wasio waaminifu wamekuwa wakihujumu miundombinu hiyo na kuwaonya kuacha mara moja kwani kwa sasa serikali imeweka mbinu mbalimbali za kuwabaini na kuwakamata, sambamba na hatua stahiki kuchukuliwa dhidi yao wanaofanya vitendo hivyo vya kuhujumu miumbombinu ya maji, ambayo serikali inatumia fedha nyingi kwa ajili ya kuinunua ili kuhakikisha mwananchi anapata huduma ya maji karibu na eneo analioishi,”alisema Mhandisi Limbe.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.