SUA-APOPO yasaini Makubaliano na Hospitali ya Kibong’oto kujenga Maabara ya Panya Buku

KIBONG’OTO-SIHA

Taasisi isiyo kuwa ya Kiserikali ya SUA-APOPO, imesaini makubaliano (MoU) na Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto kwa ajili ya kuanza ujenzi wa maabara ya panya, itakayohudumia wahisiwa wa vimelea vya Kifua Kikuu katika mikoa ya Kaskazini.

Mratibu wa SUA-APOPO, Dk Joseph Soka, aliyasema hayo jana wakati wa kusaini makubaliano hayo na kusema kuwa mradi huo unalenga kuboresha mbinu za kugundua na kutibu kifua kikuu kwa njia ya kisasa na haraka zaidi.

Dk. Soka alisema kuwa maabara hiyo itagharimu takribani Sh Bilioni 1, ambapo pia itahusisha ajira ya watumishi 12, kutoa mafunzo kwa waratibu wa kifua kikuu pamoja na watumishi wa afya ili kuboresha ufanisi wa kugundua kifua kikuu kwa usahihi.

“Leo SUA-APOPO tumeingia makubaliano na KIDH, ili kuanza ujenzi wa maabara ya panya buku, ambayo itagharimu jumla ya Sh takribani bilioni 1, maabara hii itakuwa ikihudumia wahisiwa wa kifua kikuu kwenye mikoa ya Arusha, Manyara, Tanga na Kilimanjarao.”alisema Dk. Soka.

Alisema mradi huo pia utahusisha vituo 40   vya mikoa ya Kanda ya Kaskazini na  kwa mkoa wa Kilimanjaro utakuwa na vituo 10 kutoka katika hospitali za wilaya ya Siha, Moshi vijijini, Manispaa ya Moshi, Same, Hai pamoja na vituo vyas afya.

Alisema “Vituo hivi vitakuwa vinakusanya sampuli za makohozi na kuvisafirisha kwenda Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto kwa ajili ya kuchunguzwa na Panya Buku pamoja na vipimo vilivyothibitishwa nchini kama vile Hudubini, GeneXpert na kuotesha kwenye vitalu vya kifua kikuu (MGITn L J).

Alisema panya buku hao wana uwezo mkubwa wa kugundua vimelea vya kifua kikuu hata kwa mtu ambaye alifanya vipimo  hospitalini  kama vile  vya Hadubini (Smear Microscopy) na mashine za kupima vina saba  mfano wa GeneXpert na vipimo vingine na kunatoa majibu kuwa hana kifua kikuu lakini panya buku hao wana uwezo wa kubaini  vimelea ambavyo mashine za hospitalini zinaweza zisibaini.

Alisema, utumiaji wa panya hao, unaweza kusaisdia kuongeza ugunduzi wa wagonjwa wengi zaidi kwani panya mmoja ana uwezo wa kugundua kama sampuli ina vimelea vya kifua kikuu kwa muda wa sekunde moja na hupima sampuli za makohozi 100 kwa muda wa dakika 20.

Alisema teknolojia mpya hiyo hiyo inaweza kutumika hata kwenye upimaji wa sampuli nyingi kutoka kwenye kundi kubwa la watu.

Akizungumzia mafunzo ya panya buku hao, Dk. Soka alisema  mafunzo yao huchukua muda wa miezi 9 hadi  mwaka mmoja  tangu akiwa  na umri wa mwezi mmoja  na anaweza kufanya kazi kuanzia akiwa na umri wa mika miwili hadi miaka 10.

“Panya buku mmoja anaweza kupima sampuli 100 kwa dakika 10 hadi 20, panya buku huwa anagundua TB kwa kunusa compound “Volatile organic compound  (VOC) ambayo ipo kwenye kimelea au bacteria  anayesababisha  kifua kikuu yaani (Mycobacterium tuberculosis) kwa kunusa VOC hiyo, lakini pia panya buku huyo anauwezo wa kutofautisha vimelea vya kifua kikuu na vimelea vingine.

Dk. Soka alisema panya buku; hawezi kuambukizwa TB kwa kuwa kabla hajanusa makohozi huwa yanachemshwa  (Autoclaved) kwenye jotoridi lenye nyuzi 100 kwa  dakika 40  joto ambalo lina weza kuuwa vimelea. 

Awali akizungumza Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Kiambukiza Kibong’oto (KIDH),Dk.  Peter Mbelele alisema utumiaji wa panya hao unaweza kusaidia kuongeza ugunduzi wa wagonjwa wengi wa wahisiwa wa vimela vya Kifua Kikuu katika mikoa ya Kanda ya Kaskazini.

Naye Mratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma Mkoa wa Kiliamnjaro Dk. Peter Nigwa, alisema Mradi huo utakwenda kuwaibua wahisiwa wengi wa ugonjwa wa kifua kikuu ambao huwa hawapatikani hususani watoto wadogo, ambao hawawezi kutoa makohozi yenye ubora unaohitajika.

Akizungumza Mtafiti upande wa Vipimiolojia kutoka Shirika la Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu kituo cha Mwanza (NIMR) Profesa Said Kapiga, alisema utumiaji wa teknolojia mpya ya panya buku itakwenda kusaidia namna ya kuwagundua watu ambao wameambukizwa na vimelea vya kifua kikuu.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto (KIDH) Dk. Leonard Subi, alisema hitaji la KIDH ni kuona ushirikiano katika mapambano dhidi ya magonjwa ya kuambukiza, hususan kwenye kifua kikuu wanayaendeleza.

Mradi huo wa kutumia wanyama aina ya panya buku unatarajiwa kuongeza ufanisi mkubwa katika tafiti mbalimbali za maradhi yanayoikabidi jamii.



Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.